Mada ya juma hili: MWANAJUMUIYA + NEMBO.

Sunday 4 February 2007
Kama ilivyo ada, kumaliza hatua moja ndiyo mwanzo wa kuingia nyingine. Baada ya kumaliza hatua ya Uongozi, juma hili tunaingia kipengele kingine cha UANAJUMUIYA na NEMBO ya Jumuiya. Katika UANAJUMUIYA tutazungumzia suala zima la ushiriki wa mtu katika Jumuiya kwamba:-


1. Je mwanajumuiya ni nani? mtu yeyote mwenye blogu au hata asiyekuwa na blogu?

2. Je tunahitaji taratibu zozote za mtu kujiunga na jumuiya? Je ni zipi hizo?

3. Kuwe na taratibu zozote za mwanajumuiya kutolewa katika Jumuiya? Taratibu gani?

4. Je kuna haja ya kuweka mipaka yoyote ya kinidhamu kwa mwanablogu? ipi?

Pamoja na kujadili suala la uanajumuiya, pia kamati imeona ni vyema kulijadili suala la Nembo ya Jumuiya katika kipindi hiki, sababu ni kwa vile Nembo ni mchoro unaohitaji kubuniwa, hivyo ni bora kazi hii itangazwe mapema ili wenye vipaji vyao waanze kushusha vitu. Mada hii ya Nembo iko huru haifungwi na muda wa juma moja inaweza ikawasilishwa wakati wowote wakati mijadala mingine ikiendelea.

Wachangiaji karibuni tena. Na wachoraji mko huru kuanza kazi ya Nembo.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 2/04/2007 |

Maoni: 25

naomba nichangie kama ifuatavyo

1. mwanajumuiya ni mta, asiye na nzania yeyote mwenye blogu; asiye na blogu atatukwaza kwani sie tutaongea kichina yeye kijapani, maelewano yatakuwa ya matatizo

2. utaratibu ni muhimu wa mtu kujiunga. hapo ni kuanzisha blogu mahususi ama kuendeleza blogu hii na kuifanya ya kuingia kwa masharti kama ya hapo juu

3. taratibu hazina nafasi endapo hoja namba moja hapo juu itakuwepo

4. mipaka ya kinidhamu ni muhimu ili tusijetengwa na jamii, hasa kwa wale watovu ambao watafanya hata wenye nidhamu waonekane hawana.

aidha naomba wataalamu wa nemo wazingatie utaifa kama vile ramanui na bendera ya taifa bila kuhusisha alama ya chama ama jumuiya yoyote isiyo ya kiserikali

naomba kuwasilisha...
samahani; namba 1. naomba isomeke mwanajumuiya ni mtanzania yeyote mwenye blogu;
Nakubaliana na hoja na maoni/mawazo ya mjomba michu ila nina mchango wa moja kwa moja kwenye hoja Na. 4.

Nidhamu ndio mwongozo adhimu katika maisha. Nidhamu kwa aslimia nyingi sana, ndio imewafanya kina bill gates kuwa hivi walivyo sasa, kuwapa heshima na utukufu kina Nyerere, Haile Selassie na Nkrumah,n.k.

Hivyo hata kwenye jumuia yetu kuna umuhimu mkubwa sana wa kutunza nidhamu ili mwisho wa siku na sisi tuwe katika mstari mnyoofu.

Ni hayo tu.
Mwenzenu natatizwa na jambo hapa naomba mnisaidie,

Mwanablogu ni nani?
Je ni yule tu mwenye kumiliki blogu au hata wadau wake? mfano watu kama kina Zermacopolo, mtimkubwa, born again pagan n.k hutoa michango ya haja bloguni bila wao kuzimiliki, je hawa ni wanablogu au sio?

Kipengele cha kwanza kinanishinda kujibu kutokana mkanganyiko ninaoupata juu ya nani mwanablogu?

Kuhusu taratibu za kujiunga, nadhani tunahitaji kuwa nazo ili mtu anapojiunga awe anajua ameingia wapi kwa ridhaa yake mwenyewe. Hili likikubalika itabidi zitungwe pia taratibu zenyewe.

Nakubaliana pia na suala la kuwa na mipaka ya kinidhamu na taratibu za kuvuliwa kwa mtu uanachama endapo ataenda kinyume na maadili.

**Hoja hizi ni zangu binafsi na si kama mwanakamati wa muda.

Naomba kuwasilisha.
  Tarehe: 6 February 2007 at 16:22 Anonymous Anonymous Anasema:
Nadhani ingawa jumuiya hii ni ya wanablogu, wako wadau wengine ambao wanafaidika na pia wanaifaidhisha jumuiya hii ambao hawana blogu. Hivyo, nasema haya kutokana na maswali ya Da Mija, nadhani uanachama unaweza kuwa wazi hata kwa akina Zemarcopolo.

Nadhani utaratibu wa kujiunga utakuwa ni kupitia tovuti ya jumuiya yetu. Kuwe na fomu ya maombi ya kujiunga. Wakati mtu akijaza fomu hiyo, kuwe na sehemu ambayo atapaswa kusoma masharti ya uanachama na mambo kama hayo, kisha atatakiwa kukubali au kukataa. Akikubali, basi ataweza kuendelea kujaza fomu ya maombi na kuituma kwa watakaokuwa wanahusika na shughuli ya kusajili wanachama.

Kwahiyo kama mtu anashirikiana nasi kwa maoni kwenye blogu, na anakubaliana na masharti ya jumuiya, sioni ubaya wa mtu huyo kuwa mwanachama.

Jumuiya ya wanablogu wa Kenya, KenyaUnlimited, ina wanachama kama mimi ambao sio Wakenya. Wanachotaka ni kuwa ukubali madhumuni na masharti ya jumuiya.

Kwa ufupi: mwanachama awe ni yule aliyekubaliana na masharti, malengo, na madhumuni ya jumuiya na kujaza fomu ya maombi kwenye tovuti ya jumuiya.

Maadili: kila mtu ana haki ya kuandika, kusema, kufanya lolote analotaka. Teknolojia hii inatupa uhuru wa kufanya hivyo. Ila naamini kuwa wengi wanaounga mkono wazo la kuwa na jumuiya wanaamini kuwa teknolojia hii inatupa pia majukumu fulani kwa jamii yetu. Sio tu inatuwezesha kusema na kuandika lolote, bali inatuwezesha kujumuika na wenzetu ili kujenga jamii bora yenye kujali haki, demokrasia, na maendeleo. Naamini kuwa jumuiya hii ndio chombo cha kutekeleza majukumu yetu kama Watanzania na binadamu kwa jamii nzima.

Tukikubaliana na hoja hiyo, basi tutakubaliana kuwa yapo maadili ambayo lazima tuyaheshimu na kuyalinda. Uzuri ni kuwa hakuna mtu atakayelazimishwa kujiunga na jumuiya. Ila atakayeona kuwa maadili tunayoyaheshimu hayamzuii kutumia blogu yake kwa manufaa, huyo atakuwa mwanachama.
Tujipongeze wanablogu kwa hatua hii.
Nimuhimu sana jumuiya ya wanablogu Tanzania tukiwa na nembo yetu pamoja na bendera wazo nzuri sana,lakini chakushangaza nilipendekeza wimbo unaotokana na hotuba ya Haile selassi nikaambiwa nijitahidi kubadilisha lugha.

Naunga mkono Ndesanjo aliyoyasema hapo juu.
naunga mkono hoja zilizotolewa na ndesanjo hapo juu kuhusu uanachama.
kuhusu suala la nidhamu naomba kuonezea kidogo.tusimamie nidhamu juu ya nyanja zote mbili kwa maana ya nini mwanachama anapaswa kufanya na nini mwanachama hapaswi kufanya.waliochangia juu wamezungumzia vizuri sana juu ya nini hakipaswi kufanywa na wanachama,hivyo naomba kusisitiza juu ya kilichobakia.kila mwanachama awe na majukumu ya kuyatekeleza ili kuendeleza jumuiya.mfano kupost essay etc.
nawakilisha.
1.Mwanajumuiya ni tule tu mwenye blogu au anamiliki blogu.
2.taratibu za kujiunga na jumuiya ni lazima aheshimi katiba ya wanajumuiya.
3.taratibu za kutolewa katika jumuiya lazima ziwepo kama vile
a.endapo mwanajuiya atakiuka sheria za jumuiya,mafanao kutumia kugha chafu.
b.kutoa habari zisizo za kweli.
c.kutishia amani
4.mipaka ni muhimu itasaidia
a.kuepusha wanajumuiya kutongozana wakati wengine wanandoa zinazoitwa takatifu au halali.
b.kutaka kujua familia au mume/meke wa mwanablogu.
c.kuheshimu imani ya mwanablogu kwa mfano kuto puuzia maneno ya rastafarian.hapa ni pale mwanablogu ambae ni rastafarian hapewe kipaumbele kwa sababu zisizo za msingi.
d.kuanza kumtumia mwanajumuiya maombi ya visa au mahitaji mengine.

Swala la nembo nakubaliana nalo asilimia 100%,Je tunahitaji wimbo?kama basi tunahitaji wimbo,wimbo wa aina gani?nilipendekeza hotuba ya Haile Selassi I,lakini nikaambiwa nijenge hoja nzito.
Jah Rastafarian.
  Tarehe: 7 February 2007 at 21:45 Anonymous Anonymous Anasema:
Luihamu:
Uwanja uko wazi. Tushawishi tuone umuhimu wa kuwa na hotuba ya Ras Tafari Haile Selassie kama wimbo wa jumuiya: a) kwanini Haile Selassie b) kwanini kiingereza.

Kama nimekuelewa, maoni yako ni kuwa mwanachama ni yule tu mwenye blogu?

Je wengine mnasemaje kuhusu hili?
mimi naona mwanachama si lazima awe mwenye blogu na sioni kwa nini lazima awe Mtanzania. Kwa maana itabidi muainishe kuwa Wale Watanzania wasiokuwa na passport ya Tanzania hawaruhusiwi?Msije mkadhani ni mimi.Mie Mtanzania halisi mwenye kutembea na passport ya Tanzania, lakini nawajua wanablogu wenye passport za nchi nyingine walioko miongoni mwetu.Sasa mtawatenga?

Mengineyo mendi mliyosema nakubaliana nayo.
Napendekeza mwanachama awe ni yeyote yule hata mzungu ili mradi aombe na kujaza fomu ya kuingia chamani/jumuiyani,(hivi neno mwanachama lilitokana na nini?)

Halafu kama mwanachama huyo atataka kugombea uongozi, basi hapo sharti awe anamiliki blogu.

Kuhusu NEMBO napendekeza herufi B isikosekane kwani kuwepo kwake kutasaidia kuitofautisha na JUWATA ya wafanyakazi.

Mengineyo nakubaliana nayo.
Kuhusu JUWATA ndio maana kwenye link ya site hii kwenye blogu yangu nimeiita JUMUWATA
JUWATA -
kamati ya sheria hebu tupeni ushauri hatuwezi kushitakiwa kwa tuhuma kuiba jina,hata kama JUWATA asili imekufa?
Ndio mzee Ndesanjo mwanachama ni yule tu mwenye blogu.

Nakubaliana na maoni Ya Da mija.
  Tarehe: 8 February 2007 at 19:53 Anonymous Anonymous Anasema:
Mwanachama: Nakubali kuhusu mwanachama sio lazima awe na blogu. Nakubali pia hoja ya Da Mija kuwa nafasi za uongozi zitolewe tu kwa wale wenye blogu. Nakubali pia hoja ya Kitururu na wengine kuwa mwanachama sio lazima awe Mtanzania ingawa ni jumuiya ya wanablogu wa Tanzania. Pengine kwenye katiba tutaweka wazi kuonyesha ni mambo gani ambao hawataweza kufanya kutokana na kutokuwa Watanzania (kama kugombea uongozi, n.k.). Nilitoa mfano kuwa niko kwenye jumuiya ya blogu za Wakenya, nimefaidika nayo. Wanachama wa jumuiya hii huko nyuma wamewahi kunisaidia kwenye mambo mbalimbali. Sioni kama niliharibu chochote kwenye jumuiya hii kwakuwa eti mimi sio Mkenya.

JUWATA/JUMUWATA: suala hili tulitafutie ufumbuzi. Je kifupi chetu kiwe JUMUWATA au JUWATA? Sidhani kama tutakuwa tunafanya kosa lolote kisheria a) mambo tunayofanya ni tofauti kabisa na JUWATA (muziki) ambayo ilikuwa ikijihusisha na masuala ya muziki b) haipo tena.

Uanachama: naamini kuwa kati ya mambo tutakayokuwa nayo ni kuwa mtu akishakubaliwa uanachama, atakuwa na nembo ya kuweka kwenye blogu yake ambayo itakuwa kama ndio kadi yake ya uanachama. Hapo ndio wachoraji tunawasubiri (Egidio, mshikaji wako New Delhi mtaarifu).

Nadhani kamati itabidi itoe ufafanuzi zaidi juu ya namna wachoraji nembo watakavyozitoa kazi zao ili zijadiliwe na kupigiwa kura.

**Maoni yangu hapa ninayatoa kama ndesanjo mwanablogu na sio mjumbe wa kamati ya muda**
Kuna mambo machache sana ambayo huwa tunayazungumza na ambayo kimsingi yanatakiwa kuchukuliwa kama mwongozo wetu. Ndesanjo, katika makala yako moja ulizungumzia kuhusu tabia ya wanablogu wa Kitanzania, ukasema wazi kuwa hawana hawafanyi hii kazi kwa lengo la kuwaambia akina fulani kuwa wamevaa nini leo au kula nini.

Ninachotaka kusema hapa ni kwamba wanablogi wa Kitanzania tayari tuna mwelekeo wetu (ingawa sisi wenyewe hatujajijua hivyo), kwahiyo suala la maadili halitatupa shida sana maana tutayaweka kulingana na mwelekeo ambao tumejiwekea.

- LUIHAMU: Tunapozungumzia habari, kwangu mimi ni kuwa tunazungumzia msomaji, muandikaji na hata anayedadidi au kuijadili. Kusema kuwa wanachama wawe wale tu wenye blogi, tutakuwa tunawanyima uhuru wasomaji wetu kushiriki katika Jumuiya yetu hivyo wanaweza kujitenga, hatuwezi kuishi kwa kusomana sisi wenyewe. Tuwe na vigezo, taratibu, masharti na code of ethics, ambayo kila atakayeikubali ataruhusiwa kuwa mwanachama.

- Suala la wimbo kwakweli linanivutia, japo ni kwa mbali kiasi (pengine kwasababu sijashawishiwa vya kutosha kama Ndesanjo), ila linanivutia, lakini wimbo wetu itabidi tuangalie uendane na maudhui ya Jumuiya, kwamfano Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania wana wimbo wao (Solidarity Forever), hakuna ubaya nasi tukawa nao.

NDESANJO - Nadhani watakaochora kazi zao zitatakiwa kuwekwa hapa kwa kisha zipewe namba halafu washiriki watakuwa wakipiga kura kwa kutaja namba fulani, mfano kazi yako ina namba 1, yangu namba 2, ya luihamu namba 3, sasa watakaokuwa wakipiga kura wanachofanya ni kuandika mimi napendekeza namba fulani basi.
Kuhusu JUWATA/JUMUWATA, sina uhakika sana kwa upande wa Jumuiya lakini nadhani itakuwa hivyo hivyo, kuwa ni marufuku kusajili Jina ambalo tayari linatumika na mtu mwingine kwa upande wa makampuni. Mambo pekee ambayo tunatakiwa kuyazingatia ni kuwa
a) Tutakuwa tunafanya kazi kama zile za JUWATA ya awali?

b). Tutajisajili wapi? maana ikiwa Jumuiya yetu itakuwa ya mtandaoni tu sioni kama kuna tatizo sana katika kutumia jina hilo.

halafu ni kaazi kubwa kweli maana hili jina kama kila ninavyofikiaria naona linaingiliana na wengine. JUWATA.....ikiwa tutataka kupunguza herufi za katikati tutaibuka na JWT....eh!! haya bwana
Uifupishe tu kuwa JUMUWATA. Au?
Nichangie kwenye jina ingawaje si mahali pake ila kwa vile hili swala limejitokeza hapa. Hili jina naona limeishaanza kuleta majadiliano, limeanza kuhusishwa na majina ya zamani. Wazo langu ni kuwa kwa vile jumuiya hii ndio inaanzishwa ni vyema basi jumuiya ikawa na jina ambalo halita leta utata au kuhusishwa na jina lingine.Maana ni kuwa utakapo anza kuhusishwa na kitu kingine hata kama huna uhusiano nacho inakuwa kazi ya ziada kuanza kuelezea tofauti zenu na maelezo yako yanaweza yakamelewesha mtu au la (sidhani kama tunahitaji kazi za ZIADA,na sidhani kama wanajumuiya wanapenda kuacha utata uedelee bila kutatuliwa) Na pia tukumbuke kuwa hata kama JUWATA imekufa?(au jina ndio limeacha kutumiwa sijui?) Lakini historia yake haipotei,hivyo jina litakuwa na historia yake sasa ili kuondokana na huu mchanganyo, mtazamo wangu jina liwe na utofauti kidogo, na ili iwe rahisi kuondokana na utata kama huu unaoanza kujitokeza. Ni wazo langu hili
Nakubaliana na Msangi Mdogo.
MWANAJUMUIYA:
Naungana na wale waliosema mwanajumuiya awe ni mwenye blogu-(si ndio jina lililopewa-Jumuiya ya WANABLOGU Tanzania).
Nilidhani MOJA ya Lengo ni kukuza idadi ya watu wanaoblogu..au?sio wasomaji tu. Asiye kuwa nayo bado hakatazwi kusoma au kutoa maoni kwenye blogu yoyote ile,ila akitaka kuwa mwanajumuiya aanzishe yake, naungana na Michuzi kwa msemo wake wa kuongea kichina na Kijapani.
NEMBO: Naunga hoja ya Msangi kuwa wabunifu wawasilishe nembobunifu zao, watu wapige kura ila nembo zipewe namba bila majina ya mbunifu, atakaye shinda ndio tuambiwe alikuwa ni nani(kazi hii kamati ya kipindi cha mpito mnaweza kuisimamia..au?)
  Tarehe: 11 February 2007 at 03:51 Anonymous Anonymous Anasema:
Ingawa nilikuwa naunga mkono jina JUWATA, nabadili msimamo wangu bila woga na kuunga mkono hoja za Ndabuli na Simon. Ni kweli kuwa jina JUWATA lina historia yake ya kipekee Tanzania hivyo sio vizuri kuleta utata kuhusu JUWATA ya muziki na JUWATA ya blogu.

Naunga mkono hoja ya Msangi ambayo Luihamu naye kauinga mkono kuhusu shindano la nembo.
Mimi bado niko kwenye kipengele cha nani ni mwanajumuiya.

Nimepata swali tena, Kwani tunaunda jumuiya wa WANABLOGU au ya WENYEBLOGU?

Bado napendekeza mwanajumuiya si lazima awe na blogu.

Naomba kuwasilisha.
Mija Shija,swali lako gumu
Mija, bila jumuiya tunaweza kuwa na wanajumuiya? au pasipo uongozi tunaweza kuwa na viongozi?ngoja kwanza,pasipo wanafunzi wa chekechea tunawezakuwa na chekechea?
Naomba kujibiwa na Mija shija Sayi.

Napendekeza mwanajumuiya ni yule tu mwenye blogu au anamiliki blogu na licha ya kumiliki blogu LAZIMA AWE ACTIVE BLOGGER.
Mmh! Rasta kumbe nawe mwanafalsafa.

Bila Jumuiya huwezi kuwa na wanajumuiya.

Bila uongozi huwezi kuwa na viongozi.

Bila wanafunzi wa chekechea huwezi kuwa na shule ya chekechea.

**Lakini Rasta kumbuka,
Jumuiya iliyo bora haijengwi na wenyejumuiya peke yake.

Uongozi ulio bora haujengwi na viongozi peke yake.(kuna washauri wao wasio viongozi)

Chekechea haijengwi na wanafunzi peke yake. (kuna wazazi na vyama mbalimbali vinavyosaidia kuunda hiyo chekechea)

Hivyo nasisitiza Mwanajumuiya si lazima amiliki blogu.