Samahani kwa kuchelewa kupandisha KIFUATACHO!

Monday 16 March 2009
Nilipata tatizo kidogo ku access site hii jana!

Nashughulikia nilichoahidi kiwe kimepandishwa jana!

Samahani kwa kuchelewa!

Karibu baadaye !

Simon.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 3/16/2009 | Maoni: 9

KATIKA KUFUFUA WAZO ZURI la JUMUWATA , baadhi ya maoni kutoka kwa BWAYA!

Thursday 12 March 2009
Nasikitika kukubali kuwa JUMUWATA ilibakia jina kinamna kwa wengi.

Chakutia moyo ni kwamba wenye uchungu wapo na naamini JUMUWATA imefufuka na tuipe punzi tu .

Kabla sijaongea sana!

Pata baadhi ya maoni ya watu kutoka katika mjadala ulioanzishwa na Bwaya na Rasta Ringo Jr Luihamu.

Ukimaliza kama wewe ni mgeni na JUMUWATA basi soma tuliyokuwa(YALIYOPITA) tunafikiria tufanye na JUMUWATA ili tusirudie kosa na endelea kukosoa na kuchangia nini kiendelee kutokea hapa.

Simon Kitururu.



G.shayo said...

Bwaya hapo umenena,mimi nilishaliuliza swali hilo mara nyingi sana lkn mimi sikupata jibu,kwa kifupi mimi hilo jambo linaniumiza sana.hebu mwenyekiti/katibu watujibu.
7/3/09 8:02 AM

Fadhy Mtanga said...

Kaka Bwaya hapo nakuangushia gwala. Umenena kitu chenye. Wakubwa inakuwaje? Si hatuyataki mambo ya alfu tisa mia sabin' na saba. Jumuiya yetu haipaswi kutokomea.
Tunapaswa kuifanyia kitu.
7/3/09 9:14 AM

Anonymous said...

Kaka Bwaya umenene,

hili jambo tulivalie njuga.asante sana kwa kujituma.

amani rasta hapa.
8/3/09 11:35 PM


Mtingwa said...

Mjadala mzuri. Kumbe mnayo organization? How do you go about it? Kwani hatuisikii!
9/3/09 4:36 AM


kamala J Lutatinisibwa said...

tumsubiri ndg kitururu atupeyake majibu kwanza
9/3/09 5:44 AM


kamala J Lutatinisibwa said...

tumsubiri ndg kitururu atupeyake majibu kwanza
9/3/09 5:44 AM


SIMON KITURURU said...

Nimesoma msuto na nitajibu!
9/3/09 7:48 AM


Bwaya said...

Nafikiri uwe ni mjadala wetu wote. Wale wapya ambao hatukuwepo wakati jumuiya inazaliwa, nao wanakaribishwa. Tuulize maswali ikibidi. Na Katibu wetu (kwa niaba ya viongozi wengine wasiojulikana walipo hivi sasa) atajaribu kujibu, kuelekeza na kuweka mambo vizuri.

Nia si kushutumu bali kujaribu kuangalia wapi tulikojikwaa ili tujisahihishe.

Labda tuanzie hapa. Kwamba jumuiya yetu imelala. Hilo halina mjadala. Sasa tujadili kipi kinakosekana na cha kufanya ili kuifufua ni kipi.

Tafadhali tusiogope mjadala.
9/3/09 1:33 PM


Koero Mkundi said...

Hivi kumbe kulikuwa na Jumuiya?
Ndio kwanza nasikia hizi habari.
Haya wale walioaminiwa na kupewa dhamana ya kuongoza mashua hiyo wajitokeze wenyewe hadharani tuwaweke kiti moto na kama wamechemsha basi wajitoe wenyewe wasisubiri kustaafishwa kwa manuafaa ya jumuiya.
9/3/09 9:11 PM


Kissima said...

Da! Kumbe kuna jumuia ya wanablog,? Ni hatua nzuri iliyokwisha kupigwa.
Hivi malengo hasa ya jumuia hii ni yapi?
Viongozi wa jumuia hii wako wapi? Namfahamu Kaka Kitururu basi.
Kuna malengo gani ya baadae kuhusu jumuia hii?
Mpaka sasa jumuia hii imeshapata mafanikio gani?
Ni vigezo gani vinazingatiwa ili mtu kuwa mwanachama?
Kuna kauli mbiu yoyote ya jumuia?
9/3/09 11:07 PM


luihamu said...

samahani fungua kurasa ya kuchangia mawazo kuhusu jumuiya ya wanablogu tanzania.

http://blogutanzania.blogspot.com/

www.ringojr.wordpress.com

N.B nimejaribu kuweka au kusambaza ujumbe huu takribani blogu 15.Naomba tusaidiane katika hili,tuhamasishe ili wengi waelewe umuhimu wa blogging na kuwa na jumuiya.

Bwaya kwa pamoja tunaweza.

amani.
10/3/09 12:59 AM


Anonymous said...

Hivi mwili unaweza kufanya kitu kinachoeleweka kama kichwa kina matatizo? Niambieni. How can it be?
10/3/09 2:37 AM


kamala J Lutatinisibwa said...

tufanye kitu kimoja muhimu. sisi wenye blog fualni zinazojikita kwenye kutafuta majibu ya changamoto tulizo nazo, tuunde jumuiya yetu ya kujitegemea

ni wazo langu tafadhalini
10/3/09 2:47 AM


Bwaya said...

Ringo, asante kwa hamasa. Ni kiu yetu sote kwamba wazo lililozaliwa mwaka 2006 lisife bila sababu.

Uhai wa Jumuiya yetu unatutegemea sisi sote. Si jukumu la watu fulani pekeyao ambao kimsingi hawatastahili lawama yoyote ikiwa mambo hayatakuwa kama inavyotarajiwa.

Tuifufue jumuiya yetu kwa pamoja.
10/3/09 2:50 AM


Bwaya said...

Kamala, sijakupata vizuri. Naomba ufafanue vizuri kwa sababu jumuiya tayari ipo na kinachofanyika ni kuifufua.
10/3/09 3:03 AM


kamala J Lutatinisibwa said...

basi tufanye juhudi za makusudi za kuifufua ili na sisi tusiokuwemo tuwemo. vinginevyo tujadili kwa mkabala mwingine. ni vyema tukawa na chombo chetu imara. basi tuunde kamati maalumu ya kuifufua kamati hiyo iwe chini ya uenyekiti wako ndugu bwaya, amina
11/3/09 12:35 AM


Bwaya said...

Kamala, nadhani tunachokifanya sasa hivi ni juhudi hizo hizo za kuifufua Jumuiya yetu. Ufufuzi huu unapofanyika kwa njia ya mijadala ya wazi inapendeza zaidi badala ya kuunda kamati kama wanavyofanya wanasiasa. [Manake tunaweza kuunda kamati ikaja na mapendekezo ambayo tunayaundia kamati ili kuja na hatua zitakazotekelezwa na kamati nyingine!]

Nadhani (kwa maoni yangu) kuwa kujadiliana kama tunavyofanya kunaweza kabisa kuifufua jumuiya hii.

Halafu Kamala ukiisha kuwa mwanablogu tu ni 'automatiki' kwamba unakuwa mwanachama wa Jumuiya hiyo (Labda taratibu zikibadilishwa). Kwa msingi huo, nawe umo japo hukuwaunablogu wakati inazaliwa mwaka 2006.

Narudia tena kwamba haipendezi tunapoanzisha vitu halafu tunaviacha vinaelea elea hivi na hatimaye vinajifia bila sababu.

Hata kama ni kweli kwamba wengi waliokuwepo enzi za 'vuguvugu' la Jumuiya hawaonekani lakini hiyo haitufanyi tuogope kushiriki ufufuzi huu kwa pamoja.

Unaonaje hapo?
11/3/09 4:08 AM


Mtingwa said...

Nimeipitia ile blogu ya Jumuiya. Iko kimya tangu mwaka juzi. Mimi nimwulize Katibu, nani mwenye access na blogu ile?
11/3/09 5:11 AM


Anonymous said...

Bwaya ni lazima tupate access ya ile blogu ili mijadala ianze au
tutumia hata hii blogu yako kuendesha mijadala.

jamani naomba tuchangie.

ringojr.
11/3/09 8:01 AM


Anonymous said...

Ringojr tupe maoni yako nini kifanyike
11/3/09 11:04 AM


Nalilia haki said...

Nakubaliana na anon wa 10/3/09 2:37AM. Tatizo linaloimaliza jumuiya yetu ni la kiuongozi zaidi. Mwenyekiti mbali na kutokufahamika kwa 'wananchi' lakini inaelekea kuna mazingira yasiyoeleweka yaliyomweka madarakani. Kwa mfano nilipokuwa nafuatilia kumbukumbu za mwenendo mzima wa uchaguzi kwenye blogu ya blogtanzania, nilibaini hitilafu kubwa. Uchaguzi ule ulifanyika kwa mizengwe ya kimaslahi ambapo nahisi msimamizi wa uchaguzi huo alizidiwa na damu.
Pamoja na malalamiko mazito yaliyotolea baada ya 'upishi' wa matokeo hayo, bado jamaa walibaki yakichekelea na kukejeli.

Ndugu zangu kinachotokea sasahivi ni matokeo ya kuchezewa kwa uchaguzi ule. Msilalamike
12/3/09 7:09 AM


kamala J Lutatinisibwa said...

nimekuelewa bwaya. japo umekosea nilianza kublog toka 2006.

sawa, tuendeleze mjadala
12/3/09 7:12 AM


Yasinta Ngonyani said...

Mimi ni mgeni kabisa sikujua kama kuna jumuiya ya wanablog. Na sijui mlikuwa mnajadili nini na kama kumekuwa kimya hivi basi inapaswa tufanye kitu nini sijui wenyeji watuambie.
12/3/09 9:09 AM

Mzee wa Changamoto said...

Amani, Heshima na Upendo kwenu nyote.
Nashukuru kaka Bwaya kwa changamoto hii. Kwangu naweza sema machache. Kwanza ni kwamba tutahitaji kujua mipaka ya nani anaweza kujiunga na jumuiya. Ninalomaanisha ni kuwa kwa kuwa nina imani kuwa wanajumuiya tutakuwa na orodha mahala fulani, tunahitaji kujua kama kutakuwa na "ratings" za blogs zetu. ni kwa kuwa kuna wenye habari za kiutambuzi, kiuchanganuzi, kijamii, misaada ya kielimu, misaada ya kijamii kwa ujumla, taswira na hata wapo ambao wao ni "strictly" ngono. Kwa hiyo kujua ni vipi tutaweza kuwa na mipaka ya nani atakuwepo kwenye jumuiya na ambaye hatakuwepo ni kwanini asiwepo. Na hapo ndipo linapokuja suala alilosema ndugu Kamala hapo juu kuwa na vi-branch vya jumuiya ambavyo vuinaendana na yale muandikayo. Na hili lina ukweli maana sisi wa changamoto, utambuzi na mijadala hatuna utendaji sawa na wale wa taswira pekee. Naamini umeliona hili. Lakini pia hata namna tunavyoshirikiana (baina ya bloggers) utagundua kuwa ni tofauti. Na kuendelea kung'ang'ania jumuiya kubwa isiyo na watu wa mtazamo mmoja ni afadhali kutengeneza ndogo itakayokuwa mfano kwa wengine na namna ambavyo tutaweza kutumia uzoefu wa hii kuendeleza hiyo KUBWA.
Nawakilisha na ntarejea kuendeleza mjadala kwa manufaa yetu sote.
12/3/09 9:25 AM

Bwaya said...

Asante Mube bila shaka Katibu atalichukua hili kama changamoto.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 3/12/2009 | Maoni: 3

Kuhusu Tulipofikia!

Monday 29 October 2007
Katiba itapandishwa siku chache zijazo ikiingiza mambo yaliyoshauriwa hapo chini.Kumbuka unaruhusiwa kuikosoa kabla ya wote kutamka tumeikubali . Ikikubalika , itapandishwa pia kwa kiingereza.
Samahani wote kwa ukimya kidogo!
Tuko Pamoja!
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 10/29/2007 | Maoni: 9

Kuhusu Aggregator!

Aggregator itakuja!

Funzo kutoka kwenye jumuiya zenye aggregator kama ya Wakenya; www.kenyaunlimited.com ; maswala haya kadhaa yanatakiwa kuwekwa sawa.


Kuwa kujenga aggregator bomba kunahitajika umiliki webhosting account yako. Kwa mfano baadhi hutumia A Small Orange, http://asmallorange.com/services/hosting/ , hasa hapa maarufu ni medium account ambayo huwa na gharama za USD 100.00 kwa mwaka.

Unahitaji kununua domain name.
Wengi wanashauri domain name inunuliwe tofauti na web hosting hasa kama unaweza kuamua kubadilisha web hosts baadaye.

Baadhii wameonekana kutumia zaidi huduma za kusajili domain names kupitia Name Cheap http://namecheap.com/ ambao wanagharimu USD 9.00 kwa a .com or .org name.

Katika ujenzi wa aggregator baadhi wamekuwa wanatumia software iitwayo Gregarius http://gregarius.net/ ambayo ni open source.


Hii ni katika kutoa mwangaza kidogo wa nini kinatarajiwa katika hili.
Wataalamu wa computer katika umati wetu mnakaribishwa kutoa hoja au hata msaada wa kimawazo au mwingine wowote!
Tunaamini wako wanajumuiya wenye mchango au mwanga zaidi katika swala.

Karibu kuchangia , kuuliza au hata kukosoa!
Tuko Pamoja!
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 10/29/2007 | Maoni: 3

TAFADHALI WEKA TANGAZO KWENYE BLOGU YAKO, LA KUWAFAHAMISHA WATU KUHUSU OMBI LA MCHANGO WA MAWAZO YAO HAPA KATIKA JUMUWATA.

Tuesday 18 September 2007
Mchango wako unahitajika sana wewe mwenye blogu na hata usiye na blogu ilikujenga muelekeo uliochangiwa na wengi na sio kikundi cha watu wachache.

Karibu uchangie, kosoa,kemea,shauri, ondoa, .... ilikupata muelekeo na jumuiya ya wanablogu Tanzania unayoweza kujivunia.


Kama unablogu tunaomba uweke tangazo la kuwafahamisha watu kuhusu ombi la mchango wao wa mawazo hapa ili liwezekuwafikia watu wengi.

KARIBUNI WOTE!
Uongozi.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 9/18/2007 | Maoni: 4

KWA WALIOSHINDWA KUFUNGUA DONDOO ZA KATIBA NA MUELEKEO WA JUMUWATA.

Thursday 13 September 2007
Endelea kupitia dondoo hizi, chambua, kosoa, ongezea, kemea , ili tupate kitu cha uhakika.......

Dondoo ni hizi hapa .Zimepandishwa kutokana na baadhi yetu kushindwa kufungua faili hapo chini.

Tuko pamoja!



KATIBA YA JUMUIYA YA WANABLOGU TANZANIA

Katiba ya JUMUWATA 2007


UTANGULIZI
Sisi WANAJUMUWATA tumeamua rasmi na kwa dhati kujenga jumuiya yetu tukizingatia misingi ya uhuru, haki na amani. Misingi hii itaweza kutekelezwa katika JUMUIYA iendeshwayo kidemokrasia ambapo uongozi wa jumuiya na wanachama wa jumuiya wanashirikiana katika kudumisha haki zote za binadamu, maadili ya mjengayo mwanadamu kufanya mazuri na kuendelea na uhuru wa habari .

Katiba hii imetungwa kwa ushirikiano wa WANAJUMUWATA wote, kwa dhumuni la kujenga Jumuiya ya wanablogu wenye nguvu ya kubadili mapotofu, kuweka wazi yaliyofichika, kuelimishana, kuburudisha na kujikwamua katika mipaka izuiayo uwezo wa mwanadamu kupata uwanja wa kusemea na kusikika duniani.


* SURA YA KWANZA



SEHEMU YA KWANZA

JUMUIYA YA WANABLOGU TANZANIA.
Ni jumuiya iunganishayo Wanablogu wenye blogu na wasio na blogu popote duniani, ambao madhumuni yao ni kuendeleza Tanzania kama nchi, Watanzania na Dunia kwa ujumla. Ni jumuiya isiyoendeshwa kibiashara , yenye lengo la kumfaidisha mwanablogu na Mtanzania mwenye kupenda maendeleo.

1.Maeneo JUMUWATA igusayo.

JUMUWATA inagusa wanablogu dunia nzima, na maeneo yote yamgusayo binadamu ,kwa nia ya kumjenga, kumelimisha, na sio kumdhalilisha. JUMUWATA haikubaliani na mwanablogu yeyote mwenye nia ya kubomoa utu wa binadamu mwingine asiye na hatia.

2.Nani ni MwanaJUMUWATA.

MwanaJUMUWATA ni mtu yeyote, kikundi chochote chenye nia ya kujenga mazuri yagusayo Tanzania na dunia kwa ujumla, kitambuliwacho na kusajiliwa na JUMUWATA, na kufuata sheria na maadili yakubaliwayo na JUMUWATA.

 Blogu na wanablogu wakubaliwao na JUMUWATA
Mtanzania yeyote mwenye blogu na asiye na blogu mwenye kukubaliana na maadili na sheria za JUMUWATA.
Mwanablogu yeyote duniani apendaye maendeleo ya Tanzania na kukubaliana na maadili/sheria za JUMUWATA

3.Uongozi wa JUMUWATA

Uongozi wa JUMUWATA uko katika ngazi tatu.
1.UONGOZI Mkuu (Mwenyekiti ,Katibu na Mweka Hazina)
2. Uongozi Kamati (Uongozi ushirikishao wanakamati wote).
3. Uongozi Mwanachama. (Huu ni uongozi umhusuo mwanajumuiya yeyote katika JUMUWATA.Tunaamini kuwa mwanablogu yeyote ana haki ya kuongoza na kusikilizwa katika JUMUWATA katika maswala ambayo yanafaidisha JUMUWATA na mwanadamu kwa ujumla.
Uongozi mwanachama utatambulika pale tu kikao kihusichasho Wanajumuwata , Uongozi Mkuu na Uongozi Kamati kitakubali kuwa jambo husika litaongozwa na Uongozi Mwanachama.

4.Kamati ziwakilishazo JUMUWATA


a. Kamati ya harakati

b. Kamati ya Ufundi na teknolojia

c. Kamati ya Mahusiano na vyombo vya habari.
d. Kamati ya Maadili na Ubora wa Blogu (Kamati ya picha)

e. Kamati ya sheria na Utunzaji wa maadili ya JUMUWATA

f. Kamati ya uenezi na uhamasishaji

g.Kamati maalumu ya uchaguzi


SEHEMU YA PILI

MALENGO MUHIMU NA MISINGI YA MWELEKEO WA JUMUWATA

5. Ufafanuzi

Lengo kuu la JUMUWATA ni kuwezesha wananchi wa kawaida kuwa na uwezo wakufikisha na kupokea ujumbe bila kufungwa na ukiritimba uliojengeka katika vyombo vingine vya habari. Inanuia kujenga jumuiya imara ya wanablogu ambao watakuwa ni mchango kwa maendeleo ya jamii kupitia uwezo wao wakuanika ujuzi na mawazo yao katika blogu zenye kuvutia na zenye ujumbe ujengao. Kuwezesha kublogu kwa ajili ya maendeleo ya jamii ni moja ya lengo kuu la JUMUWATA.

6.Shughuli za JUMUWATA

* JUMUWATA inaunganisha wanablogu wapenda maendeleo ya Tanzania na dunia kwa ujumla. Wanajumuwata wanaamini umoja ni nguvu na jumuwata ni chombo cha kuunganisha nguvu za wanablogu kwa nia yakupiga hatua mbele, kimaendeleo, kifikira na kiubinadamu.

* Jumuwata kwa kupitia nguvu za wanajumuwata, itaendesha miradi itokanayo na fikira na busara zitolewazo katika blogu za JUMUWATA, ilikugusa na kujenga jamii pale ilipo.(Mfano miradi igusayo jamii kwa njia ya vitabu, miradi isaidiayo watoto yatima, miradi ya kuhamasisha jamii kupata njia za kutatua matatizo yao, nk.)

* Kuwapamotisha Watanzania duniani kote kujishughulisha kifikira na kwa uwezo wao wowote kusaidia miradi ya kusaidia Tanzania.

* Kuwezesha wanablogu wa Tanzania kusikika katika jamii.

7.Kuitangaza JUMUWATA

Ni jukumu la kila mwanajumuwata kuitangaza JUMUWATA. Blogu za JUMUWATA zinatakiwa kuweka nembo ya JUMUWATA. Vyombo vya habari kama magazeti, luninga nk ;havitasahaulika katika kutangaza JUMUWATA.

8.Utekelezaji wa shughuli za JUMUWATA

Shughuli za JUMUWATA zitatekelezwa kupitia uongozi wa JUMUWATA, kamati za JUMUWATA, na wanachama wa JUMUWATA kwa kushirikiana.



SEHEMU YA TATU:

HAKI.

7.Haki za wanaJUMUWATA

Wanajumuwata wote ni sawa. Mwanajumuwata yeyote ana haki ya kutoa mawazo na kukosolewa katika JUMUWATA. Mwanajumuwata yeyote mwenye umri zaidi ya miaka kumi na nane anahaki ya kuwa kiongozi wa JUMUWATA.

8. Haki ya kupata elimu na kuelimisha katika JUMUWATA

Tunaamini kuwa kila mwanajumuwata analo la kumfunza na lakujifunza kutoka kwa mwingine. Mwanajumuwata yeyote anahaki yakufunza na kufunzwa katika JUMUWATA.

9. Haki ya kutamka,uhuru wa mawazo na kuwa na sauti ndani ya JUMUWATA

Mwanajumuwata anahaki ya kutamka lolote na kuwa na sauti ndani ya JUMUWATA iwapo tu haki hiyo haitumiki kumtukana mtu, kujenga ubaguzi wa rangi ,umri , jinsia nk. Haki ya kutamka, uhuru wa mawazo na kuwana sauti ndani ya JUMUWATA itaheshimika tu pale itumikapo kujenga na sio kumdhalilisha mtu au watu kwania ya kujenga chuki na sio kujenga jamii bora.

10.Haki ya Kuongoza , na kukataa Uongozi wa JUMUWATA

Kila mwanajumuwata ana haki ya kuongoza na kukataa kuongoza. Kila mwanajumuwata ana haki ya kuukataa uongozi, haki ambayo anaweza kuifikisha kwenye kamati maalumu ya sheria na utunzaji wa maadili, kwa kujadiliwa na mapendekezo zaidi yashirikishayo wanajumuwata wote.





SEHEMU YA NNE:

WAJIBU

11.Wajibu wa kushiriki katika shughuli za JUMUWATA

Ni wajibu wa kila mwanajumuwata kushiriki katika shughuli za JUMUWATA kama zipendekezwavyo na JUMUWATA.

12.Wajibu wa kutii sheria za JUMUWATA.

Ni wajibu wa kila mwanaJUMUWATA kutii sheria zilizokubaliwa na JUMUWATA ambazo zimepitishwa kwa kushirikisha maamuzi ya wanajumuwata wote.

13.Wajibu wakulinda mali za JUMUWATA

Ni wajibu wa wanajumuwata kuwa na uchungu na mali za JUMUWATA na kuzilinda . Adui wa mali za JUMUWATA aliye ndani au nje ya JUMUWATA ni adui wa wapenda maendeleo ya JUMUWATA.

14.Wajibu wa kulinda sifa nzuri ya JUMUWATA.

Ni wajibu wa kila mwanajumuwata kuzilinda sifa nzuri za JUMUWATA. Ni wajibu wa JUMUWATA kusaidia kuondoa au kubomoa yale yawezayo kuletea JUMUWATA sifa mbaya.




SEHEMU YA TANO:

15. MAMBO YA KUZINGATIA KWA MWANAJUMUWATA

a. Gharama za JUMUWATA hazitamuathiri mwanajumuwata binafsi katika maswala yahusuyo kushitakiwa JUMUWATA , kudaiwa fedha kutokana na shughuli za JUMUWATA
b. Kiongozi wa JUMUWATA hata daiwa binafsi kulipia shughuli zilizopitishwa kikatiba na wanajumuwata kwa kukubaliana.
c. Kiongozi wa JUMUWATA atadaiwa akitumia mali za jumuwata kiuzembe na kwa makusudio binafsi
d. Kiongozi mpya wa JUMUWATA hatahusishwa na mapungufu ya fedha na mali za jumuwata yaliyotokea kabla ya kushika kwake uongozi.
e. Katiba hii inatakiwa kufuatwa na yeyote atakaye kujiunga na ambaye ni mwana JUMUWATA
f. Atakayegundulika kwenda kinyume na maadili ya JUMUWATA , atapewa onyo na kuombwa ajitetee.Hatima itakuwa ni kuondolewa katika JUMUWATA kwa kipindi kitakacho amuliwa na wanajumuwata.
g. Mwanajumuwata atolewaye kwenye jumuwata atatakiwa arudishe mali zozote za JUMUWATA ikiwa ziko mikononi mwake.






* SURA YA PILI

MUUNDO WA JUMUWATA


SEHEMU YA KWANZA:

MWENYEKITI

16. Mwenyekiti wa JUMUWATA

Ni kiongozi mkuu wa maswala yote yahusuyo JUMUWATA.

17.Shughuli za Mwenyekiti katika JUMUWATA

* Atasimamia vikao vyote vikuu vya JUMUWATA .Anaruhusiwa kuingia katika vikao vyote vya kamati za JUMUWATA iwapo wanakamati hawana kipingamizi.
* Anawakilisha maswala yote ya JUMUWATA ambayo hakuna kamati maalumu inayasimamia moja kwa moja.
* Ni msemaji mkuu wa maswala yaihusuyo JUMUWATA.
* Ni wajibu wake kujua maswala ya uwezo wa JUMUWATA kifedha, kikuwakilisha wanajumuwata, nk.
* Ni muweka sahihi mkuu katika maswala na vyeti vyote vihusuvyo JUMUWATA.

18.Mamlaka na utekelezaji wa shughuli za Mwenyekiti

Mamlaka ya mwenyekiti huyapata tu pale ashindapo katika uchaguzi na kukabidhiwa uongozi rasmi. Utekelezaji wa shughuli za mwenyekiti unatakiwa uwe wazi kwa wanajumuwata.

19.Uchaguzi wa Mwenyekiti

Uchaguzi wa mwenyekiti utafanyika kwa kawaida pamoja na uchaguzi mkuu wa viongozi wengine.Uchaguzi wadharura waweza kufanyika pale Mwenyekiti ajiudhurupo au kutakiwa kujiengua kutokana na kukiuka maadili ya JUMUWATA.

20. Sifa za mtu kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti

Mwenyekiti wa JUMUWATA ni mwanajumuwata yeyote mwenyeblogu atakayegombea , mwenye umri wa miaka kumi na nane au zaidi. Mwenyekiti anatakiwa aonyeshe moyo wa kutaka kuendeleza JUMUWATA, Aonyeshe kuwa anauwezo wa kuendesha jumuiya.Ni yule atakayeshinda kwa kura halali za wanajumuiya.

21.Haki ya kuchaguliwa tena.

Mwenyekiti anahaki ya kugombea tena kiti hicho kihalali kama wanajumuiya hawana kipingamizi na wanaridhika na kazi aliyofanya.

22.Utaratibu wa uchaguzi wa Mwenyekiti

Uchaguzi wa Mwenyekiti utafuata taratibu za kawaida za uchaguzi wa JUMUWATA. Mwanablogu atakaye Uenyekiti, anahitajika kuwakilisha jina na picha yake . Atatakiwa ajieleze ni kwanini anafikiria yeye ni bora kuongoza JUMUWATA. Baada ya hapo atasubiri upigaji kura kama utakavyoandaliwa na kamati maalumu ya uchaguzi. Wapiga kura ndio waamuzi wakuu katika uchaguzi.

23.Wakati na muda wakushika madaraka ya Uenyekiti.

Muda wa kushika madaraka ni miaka miwili.Mwenyekiti anawezakujiudhuru au kuenguliwa kwa mujibu wa katiba.

24.Masharti ya kazi ya Uenyekiti.

Mwenyekiti hataruhusiwa kuwa katika kamati ya uchaguzi iwapo ananuwia kugombea Uongozi tena. Ni mtunzaji mkuu wa JUMUWATA, hatakiwi kuigeuka JUMUWATA akiwa ofisini.

25.Kiapo cha Mwenyekiti wa JUMUWATA.

Mwenyekiti ataapishwa kwa kiapo cha kukiri kufuata katiba ya JUMUWATA.




SEHEMU YA PILI

KATIBU

26.Katibu wa JUMUWATA

Katibu wa JUMUWATA ni mtekelezaji mkuu wa maswala yahusuyo JUMUWATA.

27.Kazi na Mamlaka yake katika JUMUWATA
* Ni karani mkuu aratibuye maswala ya JUMUWATA.
* Atahudhuria vikao vyote vikuu vya JUMUWATA na kunukuu yote muhimu yawakilishwayo kikaoni.
* Ataletewa na kuhifadhi yaleyote yatakayo jadiliwa katika vikao vyote vya kamati za JUMUWATA.
* Ni mtunza rekodi za maswala yote yahusuyo JUMUWATA.
* Ataongoza vikao vya JUMUWATA ikilazimu akishirikiana na Muweka hazina iwapo Mwenyekiti hakuweza kuhudhuria.
* Anauwezo wakuwakilisha JUMUWATA kwa kuweka sahihi katika makala na vyeti vyote vihusuvyo JUMUWATA.
* Atashiriki katika maswala yote mengine atumwayo na Mwenyekiti au Vikao vya JUMUWATA , yasiyolengwa na kamati maalumu za JUMUWATA.

28.Uchaguzi wa Katibu

Uchaguzi wa katibu utafanyika kwa kawaida pamoja na uchaguzi mkuu wa viongozi.Uchaguzi wadharura waweza kufanyika pale katibu ajiudhurupo au kutakiwa kujiengua kutokana na kukiuka maadili ya JUMUWATA.

29.Sifa za mtu kuchaguliwa kuwa Katibu
Katibu wa JUMUWATA ni mwanajumuwata yeyote mwenyeblogu atakaye gombea , mwenye umri wa miaka kumi na nane au zaidi. Katibu anatakiwa aonyeshe moyo wa kutaka kuendeleza JUMUWATA. Aonyeshe kuwa anauwezo wa kuendesha jumuiya.Ni yule atakayeshinda kwa kura halali za wanajumuiya.


30.Haki ya kuchaguliwa tena

Katibu anahaki ya kugombea tena kiti hicho kihalali kama wanajumuiya hawana kipingamizi na wanaridhika na kazi aifanyayo.

31.Utaratibu wa uchaguzi wa Katibu

Uchaguzi wa katibu utafuata taratibu za kawaida za uchaguzi wa JUMUWATA. Mwanablogu atakaye kugombea ukatibu, anahitajika kuwakilisha jina na picha yake . Atatakiwa ajieleze ni kwanini anafikiria yeye ni bora kuongoza JUMUWATA. Baada ya hapo atasubiri upigaji kura kama utakavyo andaliwa na kamati maalumu ya uchaguzi. Wapiga kura ndio waamuzi wa mwisho wa uchaguzi.


32.Wakati na muda wakushika madaraka ya Ukatibu.

Muda wa uongozi ni miaka miwili. Katibu anaweza kujiudhuru au kuenguliwa kwa mujibu wa katiba.

33.Masharti ya kazi ya Ukatibu.

Katibu hataruhusiwa kuwepo katika kamati ya uchaguzi iwapo ananuia kugombea tena uongozi wa JUMUWATA. Ni mtunzaji wa JUMUWATA, hatakiwi kuigeuka JUMUWATA akiwa ofisini. Kuigeuka JUMUWATA ni kujitoa kwake kwenye uongozi wa JUMUWATA.

34.Kiapo cha Katibu wa JUMUWATA

Katibu ataapishwa kwa kiapo cha kukiri kufuata katiba ya JUMUWATA.




SEHEMU YA TATU

MUWEKA HAZINA:

35.Muweka Hazina

Ni muhusika mkuu wa maswala yote yahusuyo fedha za JUMUWATA.






36.Kazi na Mamlaka yake katika JUMUWATA

* Nimtunza fedha na rekodi zote zihusianazo na fedha za JUMUWATA.
* Ni msimamizi wa shughuli zote za ukusanyaji wa michango na shughuli nyingine zote zihusianazo na uingizaji fedha kwa JUMUWATA.
* Ni mkuu wa maswala yakutambua vyanzo vya fedha na kusimamia mipango ya upatikanaji wa michango au fedha na mali hizo.
* Msimamizi wa akaunti za JUMUWATA. Anahakikisha na kuweka sawa maswala ya mapato na matumizi a JUMUWATA yanaenda ipaswavyo katika kutimiza shughuli na miradi ya JUMUWATA.
* Ni muhusika wakutengeneza repoti ya fedha, kwenye mkutano mkuu au hata kwa kikundi cha WANAJUMUWATA itokeapo wapo watakao kujua maswala ya mapato na matumizi ya JUMUWATA.
* Atawajibika kuwakilisha ripoti ya mapato na matumizi pia mwishoni mwa kipindi chake cha uongozi au akiwa anajiudhuru kabla ya muda wa uongozi wake kufika.
* Anahakikisha kuwa mwenyekiti anajua hali ya kifedha ya JUMUWATA mara kwa mara.
* Ataandaa bajeti ya JUMUWATA kutokana na yale JUMUWATA itakayopanga kufanya kwa kipindi cha mwaka.


37.Uchaguzi wa Muweka Hazina

Uchaguzi wa muweka hazina utafanyika kwa kawaida pamoja na uchaguzi mkuu wa viongozi wengine.Uchaguzi wadharura waweza kufanyika pale muweka hazina ajiudhurupo au kutakiwa kujiengua kutokana na kukiuka maadili ya JUMUWATA.

38.Sifa za mtu kuchaguliwa kuwa Muweka Hazina

Muweka hazina wa JUMUWATA ni mwanajumuwata yeyote mwenyeblogu atakaye gombea , mwenye umri wa miaka kumi na nane au zaidi. Muweka hazina anatakiwa aonyeshe moyo wa kutaka kuendeleza JUMUWATA. Aonyeshe kuwa anauwezo wa kuendesha jumuiya hasa katika maswala ya fedha na uongozi kwa ujumla. Ni yule atakayeshinda kwa kura halali za wanajumuiya.

39.Haki ya kuchaguliwa tena

Muweka hazina anahaki ya kugombea tena kiti hicho kihalali kama wanajumuiya hawana kipingamizi na wanaridhika na kazi aifanyayo.

40.Utaratibu wa uchaguzi wa Muweka Hazina

Uchaguzi wa Muweka hazina utafuata taratibu za kawaida za uchaguzi wa JUMUWATA. Mwanablogu atakaye kugombea uweka hazina, anahitajika kuwakilisha jina na picha yake . Atatakiwa ajieleze ni kwanini anafikiria yeye ni bora kuongoza JUMUWATA. Baada ya hapo atasubiri upigaji kura kama utakavyoandaliwa na kamati maalumu ya uchaguzi. Wapiga kura ndio waamuzi wa mwisho wa uchaguzi.

41.Wakati na muda wakushika madaraka ya Uweka Hazina

Muda wa uongozi ni miaka miwili. Muweka hazina anaweza kujiudhuru au kuenguliwa kwa mujibu wa katiba.

42.Masharti ya kazi ya Uweka Hazina

Muweka hazina hataruhusiwa kuwepo katika kamati ya uchaguzi iwapo ananuia kugombea tena uongozi wa JUMUWATA. Ni mtunzaji wa JUMUWATA, hatakiwi kuigeuka JUMUWATA akiwa ofisini. Kuigeuka JUMUWATA ni kujitoa kwake kwenye uongozi wa JUMUWATA.

43.Kiapo cha Muweka Hazina

Muweka hazina ataapishwa kwa kiapo cha kukiri kufuata katiba ya JUMUWATA.




SEHEMU YA NNE


44.Kamati za JUMUWATA

a. Kamati ya harakati

Kamati ishughulikiayo utangazaji na upelekaji wa elimu na mafunzo yawafaayo wananchi yapatikanayo katika blogu za JUMUWATA kufikia jamii. Kamati hii itashughulikia miradi itokanayo na Jumuwata kufanyiwa kazi katika maeneo yagusayo jamii moja kwa moja .(Mfano :kutoa mafunzo madarasani na katika jamii kwa njia ya uso kwa uso au kwa kutumia vitabu,pamfleti,videonk.,kuhudumia watoto wa mitaani, kuhamasisha usafi, kupanda miti nk.).

b. Kamati ya Ufundi na teknolojia
Kamati hii huhusika na:
* Ufundi utumikao kuboresha blogu na pia mambo mapya ya teknolojia yawezayo kuboresha blogu za wanaJumuwata.
* Itakuwa na majukumu ya kuwezesha mikutano ya JUMUWATA katika mtandao.
* Kusaidi kushauri waanzao kublogu
* Kutupa taarifa mpya za tekinolojia huru ambazo zitasaidia kuboresha blogu zetu
* Kupeleka elimu ya blogs mashuleni nk ikishirikiana na kamati ya harakati.
* Kutengeneza na kuhudumia kikusanya habari(aggregator)
* Kuunda na kuimarisha tovuti ya jumuiya.
* Kutoa elimu ya kutengeneza blogu kwa atakayependa






c. Kamati ya Mahusiano na vyombo vya habari.
Kamati hii itahusika na kujenga uhusiano wa Wanablogu wa JUMUWATA na vyombo vya habari, vya Tanzania na Dunia. Itahusika kuandaa habari muhimu ambazo JUMUWATA inapendelea ziwafikie Wananchi kwa kutumia vyombo vingine vya habari kama vile TV,na magazeti.Itahusika kuhakikisha jina la JUMUWATA halichafuliwi na vyombo vingine vya habari.



d. Kamati ya Maadili na Ubora wa Blogu (Kamati ya picha)

Kamati hii itashughulikia uboreshaji wa blogu za JUMUWATA hasa katika maswala ya matumizi ya picha na uboreshaji wa taaluma ya picha , video na mengineyo yahusuyo uboreshaji wa blogu ili kuzipa nguvu zaidi katika uelimishaji jamii na pia kurahisisha ujumbe kufikia jamii.

e. Kamati ya sheria na Utunzaji wa maadili ya JUMUWATA

Kamati hii huhakikisha kuwa sheria na maadili ya JUMUWATA yanafuatwa na wanaJUMUWATA. Pia hufuatilia na kuweka wazi maswala ya kisheria ambayo yanaweza kumkumba mwanablogu. Itahusika pia na kuandaa hatua za kuwaengua viongozi na wanajumuwata kama wanakiuka maadili na sheria zichungazo JUMUWATA.

f. Kamati ya uenezi na uhamasishaji

Kamati hii inashughulikia maswala ya kupata wanablogu wapya na kusaidia kuwaamsha wanablogu wanaolala na kuacha kublogu. Kamati hii itahusika pian a kuelezea manufaa ya kublogu kwa jamii.

g. Kamati maalumu ya uchaguzi

Kamati hii itashughulikia maswala yote ya uchaguzi wa viongozi wa JUMUWATA. Itahusika pia na mapendekezo ya uchaguzi wa miradi itakayotakiwa kupewa kipaumbele na JUMUWATA katika kipindi husika.



45.Uteuzi wa wanaKAMATI

Wanakamati watagombea uanakamati kwa kuwasilisha majina na picha zao na picha zao kwa wanajumuwata kuwakubali. Wanakamati pia wanaweza kupendekezwa na wanajumuwata waaminio uwezo wao katika kushughulikia kamati zihusikazo.






46.Sifa za kuchaguliwa kuwa Mwanakamati.

Mwanakamati anaweza kuwa ni mwanablogu mwenyeblogu au ambaye hana. Ambaye hana blogu anatakiwa awe anatambulika na anajulikana kwa jina lake halisi. Anatakiwa aonyeshe moyo wa kutaka kuendeleza JUMUWATA. Aonyeshe kuwa anauwezo wa kuendesha maswala ya kamati na anaaminika.

47.Haki yakuchaguliwa tena

Mwanakamati anahaki yakupendekeza au kupendekezwa jina lake tena kushika uwanakamati .Wanajumuwata kwa kura wataamua.

48.Masharti ya kazi za Uwanakamati.

Mwanakamati hataruhusiwa kuwepo katika kamati ya uchaguzi iwapo ananuia kugombea uongozi wa JUMUWATA. Ni mtunzaji wa JUMUWATA, hatakiwi kuigeuka JUMUWATA akiwa ofisini. Kuigeuka JUMUWATA ni kujitoa kwake kwenye uongozi wa JUMUWATA.

49.Kiapo cha Mwanakamati

Mwanakamati ataapishwa kwa kiapo cha kukiri kufuata katiba ya JUMUWATA.

50.Wakati na muda wakushika uwanakamati

Muda wa uongozi ni miaka miwili. Mwanakamati anaweza kujiudhuru au kuenguliwa kwa mujibu wa katiba.




SEHEMU YA TANO

MENGINEYO KATIKA UTARATIBU WA SHUGHULI ZA JUMUWATA:

51.Hazina ya JUMUWATA

Nchi akaunti za JUMUWATA zitakapo kuwepo.


Mali nyingine za JUMUWATA

52.Vianzo vya pato la JUMUWATA

* Michango ya watu binafsi
* Michango ya wanablogu
* Michango kutoka katika mashirika
* Michango kutoka serikalini
* Zawadi



53.TARATIBU za uhakiki wa fedha za JUMUWATA

* ODITA

Odita atapendekezwa kwenye kikao kikuu na atakuwa ni mtu asiye husika moja kwamoja na JUMUWATA

54.Vikao vya JUMUWATA

* Vikao vikuu


* Vikao vya dharura
#Hivi ni vikao vitakavyo itishwa pale mambo muhimu yatakapojitokeza kabla ya tarehe ya mkutano mkuu kufika.

* Vikao vya kamati

Vikao vya kamati vitafanyika na kuandaliwa na wanakamati wa kamati husika .Wanakamati watatakiwa kufanya vikao kabla ya vikao vikuu vya JUMUWATA ilikufikisha maswala ya kamati katika vikao vikuu kujadiliwa.

55.Tarehe muhimu za JUMUWATA



56.Zawadi kwa bloggers
* Blogu bora ya kisiasa
* Blogu bora ya kifalsafa na maudhui ya kimaisha
* Blogu bora ya sanaa
* Blogu bora ya picha
* Blogu bora ya fasheni
* Blogu bora ya marafiki wa JUMUWATA
* Blogu bora ya maadili ya kiufundi na teknolojia
* Blogu bora ya maswala ya Kilimo
* Blogu bora ya maswala ya jamii
* Blogu mpya bora
* Blogu ya mwaka
* Bloga wa mwaka
* Blogu bora ya mapishi
* Blogu bora ipendezayo
* Blogu bora kiufundi






SEHEMU YA SITA

57. UVUNJWAJI WA JUMUWATA:

a.JUMUWATA itavunjwa na kikao kitakacho wasilishwa na zaidi ya wanajumuwata zaidi ya robo tatu wenye kuamua kuwa JUMUWATA hainamanufaa kuendelea.

b. Baada ya kuvunjwa mali zote za JUMUWATA zitasambazwa kwa mirad isiyobinafsi yenye kufaidisha jamii kwa ujumla.

58. UHALALI.
a.Mikataba na vyeti vyote muhimu vitahitaji sahihi za viongozi wawili. Kutokana na wanajumuwata kusambaa duniani. Mwenyekiti atapewa uwezo wakuchagua viongozi ambao wanapatikana katika ngazi tatu za JUMUWATA kuweka sahihi katika mikataba au vyeti muhimu vya JUMUWATA.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 9/13/2007 | Maoni: 27

Tafakari na changia kuhusu Kamati za JUMUWATA

Tuesday 11 September 2007
Kuna umuhimu wa kuzipitia hizi kamati na kuchangia maoni yakuzijenga au hata kuzibomoa.

Tunahitaji kuzijenga hizi kamati ili kurahisisha ufanyaji kazi wa JUMUWATA. Itasaidia kuwezesha shughuli kuenda muruwa. Lakinni kabla ya kuzianzisha tunahitaji maoni ya kuziweka zijengeke vyema.

Kumbuka kuanzia jina la kamati laweza kubadilishwa ukiwa na hoja ya kulisahihisha.

Changia hata kamati mpya kama unafikiri inahitajika.

Angalia hizi hapa chini halafu changia .

a. Kamati ya harakati

Kamati ishughulikiayo utangazaji na upelekaji wa elimu na mafunzo yawafaayo wananchi yapatikanayo katika blogu za JUMUWATA kufikia jamii. Kamati hii itashughulikia miradi itokanayo na Jumuwata kufanyiwa kazi katika maeneo yagusayo jamii moja kwa moja .(Mfano :kutoa mafunzo madarasani na katika jamii kwa njia ya uso kwa uso au kwa kutumia vitabu,pamfleti,videonk.,kuhudumia watoto wa mitaani, kuhamasisha usafi, kupanda miti nk.).

b. Kamati ya Ufundi na teknolojia
Kamati hii huhusika na:
Ufundi utumikao kuboresha blogu na pia mambo mapya ya teknolojia yawezayo kuboresha blogu za wanaJumuwata.
Itakuwa na majukumu ya kuwezesha mikutano ya JUMUWATA katika mtandao.
Kusaidi kushauri waanzao kublogu
Kutupa taarifa mpya za tekinolojia huru ambazo zitasaidia kuboresha blogu zetu
Kupeleka elimu ya blogs mashuleni nk ikishirikiana na kamati ya harakati.
Kutengeneza na kuhudumia kikusanya habari(aggregator)
Kuunda na kuimarisha tovuti ya jumuiya.
Kutoa elimu ya kutengeneza blogu kwa atakayependa






c. Kamati ya Mahusiano na vyombo vya habari.
Kamati hii itahusika na kujenga uhusiano wa Wanablogu wa JUMUWATA na vyombo vya habari, vya Tanzania na Dunia. Itahusika kuandaa habari muhimu ambazo JUMUWATA inapendelea ziwafikie Wananchi kwa kutumia vyombo vingine vya habari kama vile TV,na magazeti.Itahusika kuhakikisha jina la JUMUWATA halichafuliwi na vyombo vingine vya habari.



d. Kamati ya Maadili na Ubora wa Blogu (Kamati ya picha)

Kamati hii itashughulikia uboreshaji wa blogu za JUMUWATA hasa katika maswala ya matumizi ya picha na uboreshaji wa taaluma ya picha , video na mengineyo yahusuyo uboreshaji wa blogu ili kuzipa nguvu zaidi katika uelimishaji jamii na pia kurahisisha ujumbe kufikia jamii.

e. Kamati ya sheria na Utunzaji wa maadili ya JUMUWATA

Kamati hii huhakikisha kuwa sheria na maadili ya JUMUWATA yanafuatwa na wanaJUMUWATA. Pia hufuatilia na kuweka wazi maswala ya kisheria ambayo yanaweza kumkumba mwanablogu. Itahusika pia na kuandaa hatua za kuwaengua viongozi na wanajumuwata kama wanakiuka maadili na sheria zichungazo JUMUWATA.

f. Kamati ya uenezi na uhamasishaji

Kamati hii inashughulikia maswala ya kupata wanablogu wapya na kusaidia kuwaamsha wanablogu wanaolala na kuacha kublogu. Kamati hii itahusika pian a kuelezea manufaa ya kublogu kwa jamii.

g. Kamati maalumu ya uchaguzi

Kamati hii itashughulikia maswala yote ya uchaguzi wa viongozi wa JUMUWATA. Itahusika pia na mapendekezo ya uchaguzi wa miradi itakayotakiwa kupewa kipaumbele na JUMUWATA katika kipindi husika.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 9/11/2007 | Maoni: 3

Dondoo ya Katiba!

Tafadhali soma dondoo ya katiba upate muelekeo wa nini kitafanyika.
Maoni yako yatasaidia kukamilisha katiba hii.

Kwa kifupi katiba iko kwa lugha mbili; Kiwahili na Kiingereza.
Kumbuka kuwa inatakiwa kugusa wanablogu wote popote duniani.

Ni muhimu kukumbuka umuhimu katiba kuchukua sura za kijamii na sheria za kimataifa. Kwa maana hiyo tunaiandika katika jinsi ambavyo ndani kwa ndani zitaweza kutatua aina
zozote za migogoro itakayoweza kujitokeza.


Lakini, kimsingi kama tutaamua kuisajili rasmi jumuiya yetu basi itachukua sheria za nchi ambayo itasajiliwa ndani yake. Tanzania ni nchi muafaka ingawa wanablogu wametawanyika dunia yote.

Kumbuka kuwa miradi ya JUMUWATA kamaitakubalika hapo baadaye itafanyika zaidi Tanzania.

Katiba kamili itapandishwa baada ya kukubaliana wote kuwa imegusa mambo yote.
Tazama dondoo hapa chini na changia, kosoa, jazia kwa kutoa maoni .

DONDOOyaKATIBAyaJUMUIYA
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 9/11/2007 | Maoni: 6

Gerald Shuma - Mshindi wa shindano la Nembo.

Tuesday 3 July 2007


Wanablogu tulikubaliana kwamba baada kupata nembo itakayo simama katika jumuiya ndipo tutakapomtangaza mbunifu wake. Leo hii nachukua nafasi hii kumtangaza Ndugu Gerald Shuma mchoraji wa nembo namba 2 iliyochukua ushindi. Hongera sana Gerald!!!
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 7/03/2007 | Maoni: 50

MATOKEO RASMI YA UCHAGUZI

Sunday 1 July 2007
Watanzania/Wanablog

Yafuatayo ni matokeo rasmi ya uchaguzi wa viongozi wa jumuia yetu. Lakini kwanza ni maelezo ya jinsi uchaguzi ulivyokwenda;

Jumla ya wagombea waliojitokeza kupiga kura ni 13. Kati ya hao mmoja kura yake iliharibika kabisa kwani alishindwa kabisa kupiga kura. Makosa mengine yaliyofanyika ni katika nafasi ya ukatibu ambapo baadhi ya wapiga kura aidha hawakukumbuka kabisa kuweka jina la waliyemtaka awe katibu au waliweka jina tofauti na mojawapo ya waliokuwa wagombea wa nafasi ya ukatibu ambao walikuwa ni Simon Kitururu, Miriam Kinunda na Yahya Poli. Kosa lingine ni kwamba wengi wa wapiga kura walisahau kupiga kura kuchagua nembo ya jumuiya. Wachache waliofanya hivyo ndio waliofanikiwa kutuchagulia nembo rasmi ya jumuiya.

Baada ya maelezo haya ndio matokeo

Nafasi ya Mwenyekiti

Ramadhani Msangi amepata kura 5

Luihamu Ringo amepata kura 4

Simon Mkina amepata kura 3

* Kosa lilikuwepo kwenye kura 1 iliyoharibika.


MSHINDI- RAMADHANI MSANGI

Nafasi ya Katibu

Simon Kitururu amepata kura 5

Miriam Kinunda (Malaquias) amepata kura 4

Yahya Poli amepata kura 1

* Makosa pamoja na kura iliyoharibika 3

MSHINDI – SIMON KITURURU


Nafasi ya Mweka Hazina

Mija Shija Sayi amepata kura 10

Egidio Ndabagoye amepata kura 2

* Kosa lilikuwa 1 tu kutokana na kura iliyoharibika

MSHINDI- MIJA SHIJA SAYI


Nembo ya Jumuiya

Kati ya watu 13 waliojitokeza kupiga kura watu 4 tu ndio waliopiga kura ya kuchagua nembo. Wote walichagua nembo namba 2. Kwa maana hiyo nembo namba 2 ndio nembo iliyoshinda.Inakuwa nembo rasmi ya jumuiya.

Kwa maana hiyo uongozi rasmi wa jumuiya yetu ni huu hapa;

MWENYEKITI- RAMADHANI MSANGI

KATIBU- SIMON KITURURU

MWEKA HAZINA- MIJA SHIJA SAYI

NEMBO NAMBA 2


Shukrani kwa nyote mliojitokeza kuchagua viongozi wa jumuiya yetu. Samahani nyingi kwa mliopata usumbufu au tatizo lolote wakati wa kupiga kura. Tuwape ushirikiano wa dhati viongozi wetu ili waliongoze vyema jahazi letu. Ahsanteni

Kwa niaba ya Kamati ya Muda

Jeff Msangi-Msimamizi mkuu wa uchaguzi.

 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 7/01/2007 | Maoni: 24

Leo na Kesho ni siku ya kupiga kura.

Friday 29 June 2007
Hayawi hayawi sasa yamekuwa, wadau na wanablogu wote karibu hapa katika kupiga kura kuwachagua viongozi wa Jumuiya yetu pamoja na nembo ya Jumuiya ambazo ziko chini kabisa katika blogu hii, uchaguzi wa nembo unaenda kwa namba chagua namba ya nembo na basi unakuwa umemaliza mchezo.

Tunaomba tuzingatie kanuni za upigaji kura ili mambo yaende kama yalivyopangwa.

Karibuni wote.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 6/29/2007 | Maoni: 0

Muulize swali mgombea.

Thursday 21 June 2007
Wadau kuanzia sasa mnaruhusiwa kumtwanga swali lolote mgombea linalohusiana na nafasi anayoomba, swali na jibu vitabandikwa hapa katika ukurasa mkuu.

Karibuni.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 6/21/2007 | Maoni: 3

Mabadiliko madogo ya siku ya kupiga kura.

Wednesday 20 June 2007
Wanablogu na wadau wote, tumefanya mabadiliko madogo juu ya siku ya kupiga kura. Hapo awali tulitangaza kwamba siku hiyo itakuwa ni tarehe 30/06/2007, siku hii iko pale pale isipokwa tumeongeza siku moja yaani tarehe 29/06/2007, hii ni kutokana na hali halisi ya upatikanaji wa kompyuta, wengi wetu ni lazima waende internet cafe au maofisini na wakati huo huo kuna vikwazo kama vya ukatikaji wa umeme n.k. Kwa hiyo tumeongeza siku moja ambayo ni ijumaa ili kutoa fursa zaidi kwa kila mtu kupiga kura kwa nafasi bila kukimbizana.

Kwa maana hiyo basi, tuna masaa 48 kamili ya kupiga kura, baada ya hapo hakuna kura zitakazoingia tena.

Asanteni.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 6/20/2007 | Maoni: 4

Jinsi ya kuanzisha blogu.

Tuesday 19 June 2007
Wanablogu, kutokana na ukweli kwamba watakaopiga kura ni wale wenye blogu pekee, uongozi wa muda wa umeona ni vema kutoa dondoo za jinsi ya kuanzisha blogu yako mwenyewe ili kila mmoja asikose nafasi ya kupiga kura.

Mzee wetu Ndesanjo ameandaa mwongozo mzuri sana wa kusaidia hili, unaweza kufungua hapa kusoma. Na kama unaona ni maelezo marefu sana na una haraka ya kufungua kwanza na kusoma baadaye, basi fungua hapa na ujaze utakayoulizwa ukikamilisha unakuwa tayari na blogu yako.

Karibuni wote katika ulimwengu wa kublogu.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 6/19/2007 | Maoni: 6

Sheria za upigaji kura 30-06-2007.

Monday 18 June 2007
Wanablogu na wadau wote, baada ya kukaa na kutafuta njia muafaka ya upigaji kura wa haki na halali, uongozi wa muda umekubaliana kwamba uchaguzi utafanywa kwa kufuata sheria zifuatazo:-

1. Kura zitapigwa kwa kutumia blogu hii kwa kupitia kidirisha cha maoni.

2. Wapiga kura ni wale wenye blogu tu, hakutakuwa na 'anonymous' hii itasaidia kudhibiti
yeyote atakayetaka kupiga kura zaidi ya mara moja.

3. Siku ya kupiga kura, maoni yote yatafichwa hadi uchaguzi utakapokwisha, hii itasaidia
kufanya mpiga kura asibadili mawazo na kumpigia mtu mwingine, baada ya uchaguzi kura
zote zitawekwa wazi. (comment moderation itatumika.)

4. Viongozi wa muda ambao wamegombea nafasi za uongozi hawatasimamia upigaji kura.
Kutakuwa na wasimamizi wengine.

Bado haijajulikana muda kamili wa kupiga kura, kwa hili tunaweza kujadiliana wote.

Asanteni.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 6/18/2007 | Maoni: 12

YAHYA POLI (KAKA POLI)- NAFASI YA KATIBU

Thursday 14 June 2007


Wasifu
Jina: Yahya Poli [Kaka Poli]
Umri: Miaka 28
Kazi: Volunteer - Kituo cha Sheria na Hakiza Binadamu,
Uhusiano: Sijaoa - Mtoto 1 [Nadia Poli]
Blogu: Nimeanza kublogu tangu mwaka 2005

Kwa nini unagombea nafasi unayoomba.

Nina dhamira ya kutumia kipaji changu cha uhamasishaji na oganaizesheni kwa kuwahamasisha watu wengi zaidi hasa wanamapinduzi kushiriki katika kublogu kwa ajili ya kuleta mapinduzi ya kweli nchini kwetu. Nini unatarajia kufanya katika kuikuza Jumuiya.Nitahakikisha nashirikiana na wadau wengine wote katika blogu ili kutimiza wajibu wangu!

Blogu: http://www.mawazo-huru.blogspot.com/
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 6/14/2007 | Maoni: 8

Tarehe ya uchaguzi 30/06/2007

Wapendwa wanablogu, kamati ya muda inapenda kuwatangazia kuwa tarehe ya uchaguzi wa jumuiya itakuwa ni 30/06/2007. Tarehe hii imefikiwa ili kutoa muda kwa wagombea kufanya kampeni zao huku na kule na kuhakikisha wanablogu na wadau wote wanapata habari juu ya uchaguzi huu.

Pamoja na hilo, pia kamati imetoa nafasi za lala salama kwa yeyote ambaye bado angependa kugombea ajitokeze, bado tunahitaji watu na tunaamini watu tunao wenye kila uwezo wa kuinyanyua jumuiya yetu.

Asanteni wote.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 6/14/2007 | Maoni: 2

EGIDIO NDABAGOYE - NAFASI YA UWEKA HAZINA.

Saturday 9 June 2007

Wasifu.

Jina: Egidio Ndabagoye
Umri: 25
Utaalamu: Uhasibu na Ushirika
Uhusiano: Sijaoa
Utaifa: Mtanzania

Sababu ya kugombea nafasi hii.

Naamini nafasi hii inatakiwa mtu mwenye taaluma ya uhasibu ili kujua mapato na matumizi na mipango endelevu ya kuendeleza jumuiya yetu na kuifanya iendane na mabadiliko ya kibiashara. Nami naona kwa kushikirikiana na wanablogu wenzangu uwezo huu wa kuiendeleza jumuiya ninao.

Naomba kura zenu

http://www.gaphiz.blogspot.com
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 6/09/2007 | Maoni: 6

MIRIAM KINUNDA (MALAQUIAS) - NAFASI YA KATIBU

WASIFU.

JINA: Miriam Kinunda (Malaquias)
UMRI: 38
UTAALAM: Teknolojia.
URAIA: Mtanzania
BLOGU TOKA: 2006
TOVUTI TOKA: 2004 .
Kwa nini Nagombania Ukatibu.
Kupewa nafasi ya uongozi naamini ni kutumikia wale walioniteua, pia kushirikiana na viongozi wengine kutekeleza maombi yanayoletwa na wale waliotuteua. Elimu yangu ya teknolojia inaweza kutumika vizuri wakati huu ambao JUMUWATA bado changa. Nitatumia uwezo wangu na elimu yangu kutengeneza blogu mpya na pia kutekeleza majukumu yeyote kusaidia tovuti ya JUMUWATA iwe imara. -JUMUWATA inahitaji viongozi wenye uwezo wa kusikiliza sauti za wanachama wote bila ubaguzi, mimi nina Uwezo wa kusikiliza sauti ya kila mtu bila kupendelea. Uwezo huu ni wa muhimu sana wakati huu ambao JUMUWATA ni bado Changa na tuna majukumu ya kuunda katiba ya jumuiya.
NAOMBA KURA ZENU.
http://blog.mirecipe.com/
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 6/09/2007 | Maoni: 16

SIMON MKINA- NAFASI YA MWENYEKITI

Wednesday 30 May 2007
WASIFU
Jina: Simon Martha MKINA
Umri: Miaka 36.
Utaalamu: Mwandishi, mchambuzi na mjasiriamali
Kazi ya sasa: Mwandishi
Uhusiano: Nimeoa na nimejaaliwa watoto wawili
Nafasi ninayogombea: Uenyekiti
Uraia: Mtanzania
Kuingia Blogu: mwaka 2004

SABABU ZA KUGOMBEA
Nimeamua kuwaomba wanablogu wenzangu kunipa fursa ya kuongoza chama chetu kwa lengo kubwa la kutetea uwepo wake, kutambulika, kuongeza wanachama, kutoa mafunzo anuai;ikiwemo ya kutambua haki zao na zaidi sana kuwa na ushirikiano mkubwa ndani ya utaratibu wa kublogu na hata masuala ya kijamii; kusaidia wakati wa shida na raha.
Mara nyingi umoja umekuwa ni nguzo muhimu katika kufanikiwa, nitafanya kila linalowezekana, kwa msaada wa wanachama wenzangu kuhakikisha chama kinakua kwa kuwa na wanachama wengi wa kada mbalimbali.

Nitatumia uwezo wangu wa kushawishi na kuhamasisha kupata njia za wazi katika kukisaidia chama kwa rasilimali ili baadaye kuwa na mtazamo wa kuanzisha miradi itakayosaidia, siyo wanachama tu, bali mama yetu Tanzania.
Katika kuyatekeleza hayo, ninaamini mimi ni DARAJA la kumfikia kila mwanachama na kumpa fursa ya kutambua nafasi yake katika kuendeleza na kuimarisha chama ambacho nitakuwa mstari wa mbele kuhakikisha kinasajiriwa na kutambulika na taasisi zote za serikali, umma, binafsi na mashirika ya kimataifa.
MATARAJIO:
Ninaamini kabisa kuwa nitapewa fursa ya kuwa kiongozi na kamwe sitabweteka na kuwa mtawala ambaye anaona dhamana aliyopewa ni bora kuliko wanachama waliomwezesha kuingia katika uongozi.
Nitawashirikisha wanachama wote kuleta maendeleo makubwa zaidi ya fikra komavu, uchumi, jamii na zaidi sana kuboresha taswira na nguvu ya mawasiliano huru ya blogu katika Tanzania.

AMINI:

MIMI NI DARAJA LA KUTETEA NA KUHAKIKISHA YOTE YANAWEZEKANA KUBORESHA AFYA YA MWILI NA AKILI KWA WATANZANIA WOTE KUPITIA VIONGOZI NA WANACHAMA WA BLOGU TANZANIA.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 5/30/2007 | Maoni: 25

MUDA UMEONGEZWA.

Saturday 26 May 2007
Kutokana na watu kutojitokeza katika kugombea nafasi za uongozi wa jumuiya, uongozi wa muda umeamua kuongeza muda hadi tarehe 9 / 06/ 2007. Hii itakuwa ni siku ya mwisho ya kupokea maombi. Wanablogu tunaomba tujitokeze kwani madhumuni ya blogu si kutoa maoni peke yake bila kutenda yale tunayoyajadili. Umefika wakati sasa wa kutenda yale tunayoyakosoaga hivyo tujitokeze.
Fungua hapa upate maelekezo ya jinsi ya kutuma maombi.

Karibuni wote.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 5/26/2007 | Maoni: 9

Ramadhani Msangi- Nafasi ya Mwenyekiti.

WASIFU
1. Umri : miaka 31
2. Utaalamu: Biashara (masoko & matangazo), Habari na Sheria
3. Sijaoa

KWANINI NAGOMBEA:
Kuweza kushirikiana na wenzangu katika kuunda Jumuiya imara itakayowawezesha Watanzania kupata taarifa na maarifa kwa ajili ya maendeleo yao, hasa katika zama hizi ambapo kuna aya za kishetani zinazopigiwa debe kwa jina la sheria za uhuru wa habari.

NINI NITAFANYA:
- Kushirikiana na wenzangu kuunda katiba kwa ajili ya Jumuiya
- Kujenga mazingira ya kuifanya Jumuiya, tegemeo la kila Mtanzania
- Kujenga mazingira ya kuwawezesha na kuwavuta Watanzania zaidi katika ulimwengu wa TEKNOHAMA (Teknilojia ya Habari na Mawasiliano).

http://www.msangimdogo.blogspot.com
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 5/26/2007 | Maoni: 4

Mija shija Sayi - Nafasi ya uweka hazina.

Tuesday 22 May 2007
Wasifu.

Umri: 34.
Utaalamu: Mtaalamu wa sanaa za jukwaani na za mikono.
Tabia: Msumbufu.

Sababu za kugombea nafasi ya hazina.

Ninaamini mwanamke ni mpangaji mzuri wa matumizi, na mimi ni mmoja wapo. Hivyo nataka kuisimamia jumuiya katika wakati huu wa awali na kuhakikisha haiyumbi wala kuyumbishwa katika kitengo cha hazina.
Zaidi ya hayo ninataka kushirikiana na wenzangu katika uundaji wa katiba ya jumuiya.

Naombeni Kura zenu.

http://www.damija.blogspot.com/
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 5/22/2007 | Maoni: 26

Simon Kitururu - Nafasi ya katibu.

Tuesday 15 May 2007

WASIFU:
Umri: Miaka 33.
Utaalamu: Mtaalamu wa biashara.

Kwa nini anagombea kuwa katibu:-

Nagombea nafasi ya Ukatibu nikiwa na dhumuni la kuimarisha jumuiyakatika kipindi hiki cha mwanzo.Ikiwa ni pamoja nakuhakikisha jumuiya inakuwa na katiba na kamati zifanyazo kazi. Najua mwanzo ni mgumu na ninaamini nina uwezo wakukabiliana na ujenzi wa jumuiya hii hasa kipindi hiki cha mwanzo cha ujenzi wa msingi imara wa jumuiya.

http://www.simon-kitururu.blogspot.com/

http://www.fikira.blogspot.com/

Naombeni kura zenu.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 5/15/2007 | Maoni: 17

Luihamu ringo - Nafasi ya Mwenyekiti

Sunday 13 May 2007

Katika kuitikia wito wa kuomba nafasi za uongozi wa Jumuiya, mwanablogu Luihamu amejitokeza tayari, yeye anaomba nafasi ya kuwa Mwenyekiti. Yafuatayo chini ni maelezo yake binafsi, malengo yake kwa jumuiya na kwa nini anataka kuwa Mwenyekiti.

WASIFU.
Kazi: Mtaalamu katika masuala ya data entry.
Umri: Miaka 28.
Utaifa: Mtanzania.


Maelezo kwa nini nagombea nafasi ninayoomba.

Kwa mtazamo wangu au dira yangu, napenda jumuiya iwe sauti ya watoto yatima.Watoto wengi wanabaki katika hali mbaya ya maisha. Hakuna wakulaumiwa bali ni sisi wenyewe kuchukuwa hatua ya kuona watoto yatima wanalelewa katika mazingira mazuri.


Nini natarajia kufanya katika kuikuza Jumuiya

1. Kuelimisha jamii kuhusu blogu. Dhana mpya ya uandishi wa habari.
2. Kukuza kamati na kuziwezesha .
3. Dira ya kujenga kituo cha watoto yatima chini ya jumuiya ya wanablogu tanzania mfano
JUMUIYA YA WANABLOGU TANZANIA KITUO CHA WATOTO YATIMA.

http://luihamu-rastafarian.blogspot.com/

Naombeni kura zenu.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 5/13/2007 | Maoni: 9

Waombaji wa nafasi za uongozi.

Saturday 12 May 2007
Katika kubooresha zaidi zoezi zima la uchaguzi wa viongozi wa Jumuiya, kamati imeona ni vyema waombaji wa nafasi hizo wawe wakituma maombi yao katika kamati na baadaye yatabandikwa katika ukurasa wa mbele.

Mambo ya kuzingatia katika uombaji:-

1. Tuma picha yako.

2. Wasifu wako.

3. Maelezo kwa nini unagombea nafasi unayoomba.

4. Nini unatarajia kufanya katika kuikuza Jumuiya.

Tuma maelezo kwa anuani hii mijasayi@yahoo.com
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 5/12/2007 | Maoni: 7

TANGAZO: Nafasi za uongozi katika jumuiya ya wanablogu Tanzania.

Sunday 6 May 2007
Jumuiya ya wanablogu Tanzania (Jumuwata) inatangaza nafasi za uongozi wa Jumuiya katika nafasi zifuatazo:-

1. Mwenyekiti

2. Katibu

3. Mweka hazina.

SIFA.

1. Awe na umri kuanzia miaka 18

2. Awe na mapenzi na harakati za blogu, si lazima awe na blogu.

Kazi kubwa ya mwanzo ya viongozi hawa itakuwa ni kuandika katiba ya Jumuiya na kuunda kamati mbalimbali kulingana na katiba itakavyokuwa ikisema. Kwa maelezo zaidi juu ya suala zima la uongozi wa jumuiya mnaweza kurejea hapa.

Zoezi hili liko wazi hadi tarehe 25 mwezi wa 5. Tarehe 26 itakuwa ni uchaguzi wa viongozi Nembo, tarehe 27 matokeo na ufunguzi rasmi wa jumuiya.

** Kwa kujiandikisha, tumia kidirisha cha maoni kuandika jina lako na nafasi unayotaka.

WOTE MNAKARIBISHWA.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 5/06/2007 | Maoni: 16

Nembo namba 4.

Saturday 21 April 2007

 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 4/21/2007 | Maoni: 3

Nembo namba 3.


 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 4/21/2007 | Maoni: 3

Nembo Namba 2.

Sunday 15 April 2007

 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 4/15/2007 | Maoni: 10

Nembo Namba 1

Saturday 31 March 2007
Wanablogu, hapa chini ni nembo ambazo zimeanza kuingia mashindanoni. Nembo hii itajulikana kama nembo namba 1. Shindano ndiyo limeanza, karibuni wote.




 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 3/31/2007 | Maoni: 5

Shindano la kubuni nembo ya Jumuiya ya wanablogu Tanzania.

Sunday 25 March 2007
Wanablogu na wasomaji wote, kama ilivyokubalika hapo awali juu ya kuwa na nembo, Sasa tunakaribisha rasmi nembo hizo. Shindano litaendeshwa hadi tarehe 30-04-2007, na zawadi itakuwa ni kuchaguliwa na kutumika kwa nembo yako. Tulikubaliana pia kuwa nembo zitakapotumwa hatatajwa mbunifu bali picha yake itapewa namba kitu ambacho kitasaidia kuepuka kuchaguliwa kwa picha kutokana na umaarufu wa mchoraji. Wote mnakaribishwa wachoraji na wasio wachoraji.

Kwa kutuma Nembo hizo tumia anuani hii: mijasayi@yahoo.com
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 3/25/2007 | Maoni: 4

Mjadala umefungwa.

Monday 12 March 2007
Leo hii imetimia miezi miwili kasoro siku mbili tangu tuanze mjadala katika blogu hii. Tulianza tarehe 13 ya mwezi wa 1, na kumaliza leo tarehe 11 ya mwezi wa 3. Ni furaha iliyoje kupiga hatua hii!

Tulipoanza tulikuwa na lengo ya kujadili vipengele vikuu sita ambavyo vitasaidia kuunda Jumuiya muafaka ya wanablogu wa Tanzania. Vipengele hivi ni pamoja na:-
1. Uundaji wa jumuiya ya wanablogu Tanzania.

2. Jina la jumuiya na aina ya muundo wake.

3. Kikusanya habari na jina lake.

4. Ujenzi wa tovuti ya jumuiya.

5. Tuzo na mfumo wa utolewaji wake.

6. Siku ya blogu Tanzania.

Leo hii kutokana na ushirikiano wenu tunashukuru tumeweza kupata msingi wa jumuiya yetu ambao ndio utasaidia kusimamisha nguzo tuzitakazo. Tukumbuke jumuiya bado haijajengwa, hii ni hatua ya kwanza iliyotupatia msingi, tutaingia hatua ya pili ambayo itatukamilishia ujenzi mzima wa jumuiya yetu.

Kwa kweli hatuna la ziada tunawashukuru kwa mawazo yenu na sasa tunatamka rasmi kwamba hatua ya kwanza ya mjadala imefungwa.
Asanteni.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 3/12/2007 | Maoni: 5

Yaliyokubalika katika mada iliyopita... ''Siku ya blogu Tanzania.

Sunday 11 March 2007
Kama ilivyo ada yetu ya kutoa hitimisho la kila mada inayojadiliwa, leo tena tunafuraha kuwaletea yaliyokubalika katika mada iliyopita iliyohusu siku ya blogu Tanzania kama ifuatavyo:-

- Wanablogu wamekubali kuwepo kwa siku ya blogu ambayo itakuwa ni kila tarehe 18 ya mwezi
wa 11, tarehe ambayo mkutano wa kwanza wa wanablogu wa Tanzania ulifanyika.

- Pamoja na siku hii, imependekezwa iwepo wiki ya wanablogu wa Tanzania ambapo katika wiki
hii zitafanyika shughuli mbalimbali za kuitangaza blogu kwa umma, shughuli kama uandishi wa
makala mbalimbali, kufanya mahojiano na vyombo vya habari kama redio, luninga na hata
maonyesho ya sanaa. Pamoja na haya yote wiki hii ambayo kilele chake ndiyo kitakuwa 18/11
itakuwa na ujumbe maalumu utakaokuwa ukiongoza shughuli nzima.

Ndugu wanablogu, hayo ndiyo yaliyokubalika lakini tunaamini yako mengi yatakayozaliwa wakati utekelezaji utakapoanza, milango iko wazi kwa mawazo zaidi wakati wowote. Asanteni.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 3/11/2007 | Maoni: 0

Siku ya Blogu Tanzania

Monday 5 March 2007
Wapenzi wasomaji na wachangiaji wote. Juma hili
tutajadili mada ya mwisho kabisa ya vipengele vikuu
tulivyokuwa tukivijadili tangu kuanza kwa mjadala huu.


Mada hii ni fupi inayohusu kuwepo au kutokuwepo kwa
siku ya blogu Tanzania. Katika mkutano wa kwanza,
ilionekana kwamba upo umuhimu wa kuwa na siku hii,
lakini ilionekana kwamba ni vyema suala hili likawekwa
bayana kwa kupewa muda wa kutosha kujadiliwa, na ndiyo
sababu leo hii tumeiweka mada hii hewani ili wote
tujadili.

Je ni vipi tutakuwa tukiienzi siku hii?

Mawazo yenu yanahitajika. Asanteni.

Labels:

 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 3/05/2007 | Maoni: 8

YALIYOKUBALIKA KUHUSU TUZO + MAJINA YA TOVUTI NA

Wapenzi wanablogu na wasomaji wote, kwa mara nyingine tena tunafurahi kuwaletea matokeo ya mada mbili zilizopita. Kama wote tunavyojua kwamba katika juma lililopita tulikuwa na mada kuu moja hii ilihusu Tuzo kwa wanablogu wa Tanzania na nyingine ambayo ilihitaji kukamilishwa hii ilikuwa ni juu ya majina ya Kikusanya habari na Tovuti.

Kutokana na ushirikiano wenu leo hii tumeweza kupata majibu ambayo tulikuwa tukiyatafuta, na tunapenda kuyawasilisha kama ifuatavyo:-
1. JINA LA TOVUTI NA KIKUSANYA HABARI.
Wanablogu wamependekeza kwamba Tovuti ichukue jina la jumuiya. Kwa hiyo basi
Tovuti hii itakuwa ikiitwa 'JUMUIYA YA WANABLOGU TANZANIA.
Kuhusu kikusanya habari, wanablogu wamependekeza kiitwe 'KUNANI BLOGUNI'.

2. TUZO.
Kuhusu Tuzo, wanablogu wote waliochangia hoja wamekubali kwa nguvu moja kuwa na Tuzo kwa wanablogu. Na imependekezwa kwamba ziwe zikitolewa katika siku ya blogu Tanzania kama siku hii itakubalika kuwepo. Kuhusu aina za Tuzo na mfumo wa utolewaji wake hili litakuwa likishughulikiwa na uongozi husika utakaokuwepo madarakani kwa wakati huo.
Ndugu wachangiaji mada, tunashukuru sana kwa michango yetu na Jiandaeni kwa mada nyingine wakati tukielekea mwisho wa mijadala.

Labels: , ,

 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 3/05/2007 | Maoni: 0

Mada ya juma hili: TUZO

Monday 26 February 2007
Kwa mara nyingine tena tunachukua nafasi hii kuwashukuru wale wote wanaofanikisha mjadala huu. Mambo yanazidi kusonga mbele, na tuna furaha kuwasilisha tena mada mpya tutakayohangaika nayo katika wiki hii nzima. Wiki hii tutajadili juu ya TUZO. Mjadala utalenga kuwa au kutokuwa na TUZO kwa wanablogu wa Tanzania. Sambamba na hili tutajadili pia MFUMO WA UTOLEWAJI wake kama tutakubaliana ziwepo. Tunahitaji kujadili kujua zitatolewaje? Kwa kupigiwa kura au? Tuzo hizi/hii itakuwa ni nini? na pia Sifa za kupata TUZO. Hatuna mengi ila tusisahau kupiga kura juu ya jina la Tovuti na Kikusanya habari cha Jumuiya hapo chini.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 2/26/2007 | Maoni: 11

Matokeo ya mada iliyopita, Tovuti na Kikusanya habari.

Sunday 25 February 2007
Juma lililopita tulikuwa katika mjadala mzito juu ya kuwa na TOVUTI na KIKUSANYA HABARI katika jumuiya yetu. Mjadala ulienda vizuri na hadi kufikia leo ambapo ndiyo mwisho wa mjadala wa mada hii wanablogu wamekubali Jumuiya iwe na Tovuti na pamoja na Kikusanya habari.

Katika mjadala huo, tulitakiwa pia tupendekeze majina ya Tovuti na Kikusanya habari kama tutakubaliana viwepo. Tumependekeza majina mbalimbali, lakini hadi sasa hivi bado halijapatikana jibu moja lililokubaliwa. Bado kuna utata katika mapendekezo ya wachangiaji ambao mawazo yao yameonekana kuungwa mkono na wengi, kwa mfano Kitururu amependekeza majina mengi, lakini yaliyoonekana kupendwa zaidi ni KIPYA BLOGUNI, wengine wakamrekebisha na kutaka iwe MPYA BLOGUNI, sasa hapo inabidi tukubaliane jina tunalolitaka. Huu ni mfano tu. Kwa hiyo kutokana na hali hii kamati inaongeza muda wa juma lingine katika mada hii. Majina yote yaliyopendekezwa yatapigiwa kura upya na kwa vile huu ni muda wa ziada, tunaomba tusiongeze majina mapya kwa kuwa muda wake umekwisha, tuunge mkono au kukataa haya tuliyonayo.

** Pia kuna habari njema tumezipata hivi punde kwamba kuna mdau mmoja ameshajitolea kugharamia gharama za TOVUTI na KIKUSANYA HABARI, wote tunafahamu vitu hivi si bure, kuna malipo katika kupata domain name na mambo kama hayo. Mungu atupe nini jamani!!
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 2/25/2007 | Maoni: 6

Mada ya juma hili: Kikusanya habari (Aggregator) na Tovuti ya Jumuiya.

Monday 19 February 2007
Naam, mambo yaenda yakipamba moto. Baada ya kumaliza juu ya katiba, sasa tunaingia katika ukumbi mwingine muhimu wa ukusanyaji habari na nyumba ya habari. Kama wote tunavyojua suala zima la blogu ni upashanaji na uchambuzi wa habari. Je habari hizi tunazipata wapi? Jibu dhahiri ni hutafutwa na kuwekwa mahala ili wasomaji wasome yanayojili kila siku.

Katika mkutano wa kwanza tulioufanya 2006, yalitoka mawazo kwamba ni vyema tuwe na tovuti ya Jumuiya na pia kikusanya habari (aggregator) hiki kitasaidia kukusanya habari za wanablogu kwa wakati mmoja na hivyo kupunguza safari za kutembelea wanablogu kujua kama wanajipya au la. Kikusanya habari huonyesha nani kaandika habari hivi karibuni na mambo mengine mengi.

Sasa wakati umewadia wa kukubali au kukataa mawazo yaliyopendekezwa juu ya kuwa na au kutokuwa vitu hivi viwili, tujadili huku tukizingatia majina ambayo tutayapa Kikusanya habari na Tovuti. Kama unaunga mkono unaruhusiwa kutoa na jina unalodhani litafaa.

karibuni wote.

**Kuna hiki kikusanya habari cha wanablogu wa Kenya unaweza kuangalia ili kuona inavyofanya kazi.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 2/19/2007 | Maoni: 26

Yaliyokubalika kuhusu KATIBA na nani ni MWANAJUMUIYA.

Sunday 18 February 2007
Haya tena ndugu wanablogu, kama ilivyo kawaida ya kila Jumapili kutoa jibu la yale yaliyokuwa yakijadiliwa katika juma zima, leo tena muda umewadia. Juma lililopita tulijadili kama Jumuiya iwe na katiba yake au la, na pia tuliendeleza mjadala juu ya nani awe Mwanajumuiya. Yafuatayo ndiyo yaliyokubalika:-

KUHUSU KATIBA.
Imekubalika kwamba jumuiya itakuwa na katiba yake. Hii itafanya Jumuiya kuwa na mwongozo maalumu na pia itasaidia katika utekelezaji wa mambo mbalimbali.

KUHUSU NANI MWANAJUMUIYA.
Kutokana na maoni ya wengi imekubalika kwamba mwanajumuiya si lazima awe anamiliki blogu. Mtu yeyote anaruhusiwa kujiunga na Jumuiya hii isipokuwa ni lazima aombe uanachama na akubaliane na masharti ya kujiunga na Jumuiya.

Kwa mara nyingine tena tunatoa shukrani kwa wote waliojitokeza kufanikisha mjadala huu. Kaa tayari kwa mada itakayofuatia.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 2/18/2007 | Maoni: 0

Mada ya juma hili: KATIBA.

Monday 12 February 2007
Juma lingine linaanza na mada mpya inaingia. Wasomaji bado tuko katika mada ya Muundo wa Jumuiya na katika juma hili tutajadili juu ya kuwa au kutokuwa na KATIBA ya Jumuiya.

Mada hii inaweza ikawa inaonekana fupi na rahisi kuijadili, lakini tunaomba tusiichukulie juu juu, tuchukue muda na kujiuliza kwanza juu ya umuhimu wa katiba, na kwa nini tunadhani jumuiya yetu inahitaji au haihitaji Katiba.

Karibuni katika mjadala. JE TUNAHITAJI KATIBA?
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 2/12/2007 | Maoni: 22

Yaliyokubaliwa kuhusu Mwanajumuiya na Nembo.

Sunday 11 February 2007
Kwanza tunawashukuru wachangiaji wote wa mada iliyopita, mada ambayo hadi kufikia siku ya leo ya kutoa matokeo bado ina kipengele kilichosimama njiapanda.

Juma lililopita tulijadili kuhusu Mwanajumuiya na taratibu zitakazomzunguka na pia tulijadili juu ya Nembo ya jumuiya kama mada ya ziada.(mada hii iko huru kuendelea).

Na kama tulivyokubaliana kwamba kila Jumapili litakuwa likitolewa jibu, basi yafuatayo ndiyo majibu yaliyokubalika.

1. Kuhusu nani awe ni mwanajumuiya.

Katika hali ambayo haikutegemewa kipengele hiki kimepata kura sawa kwa sawa na
kufanya kukosa jibu kamili hadi sasa hivi.

Kuna wachangiaji ambao wamependekeza kwamba mwanajumuiya ni lazima awe na blogu
yake mwenyewe hawa ni Michuzi, Kaka Pori, Ras Luihamu na Ndabuli.

Vilevile kuna wachangiaji ambao wamependekeza kwamba mwanajumuiya si lazima awe
na blogu yake mwenyewe na hawa ni Kitururu, MsangiMdogo, Ndesanjo na Da'Mija.

Kwa maana hiyo basi, kipengele hicho itabidi kipigiwe kura ili kupata kundi lenye
watu wengi zaidi.

2. Kuhusu taratibu za mtu kujiunga na kusimamishwa katika jumuiya.

Katika kipengele hiki wachangiaji wote wamekubali kuwepo na taratibu hizi ili
kulinda nidhamu ya jumuiya na utendaji kazi wake.

Kwa maana hiyo kutakuwa na mipaka ya nidhamu ya Jumuiya itakayoundwa na wanajumuiya wenyewe pale jumuiya itakapoanza Rasmi.

Ndugu wasomaji na wachangiaji, tunashukuru kwa mchango wenu na tunapenda kutangaza kwamba mada hii imefungwa isipokuwa kipengele cha nani anapaswa kuwa mwanajumuiya. Kipengele hiki kitaendelea hadi kura nyingi zinazopendekeza upande mmoja zipatikane.

Karibuni kwa mada ya Nani awe mwanajumuiya.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 2/11/2007 | Maoni: 9

Mada ya juma hili: MWANAJUMUIYA + NEMBO.

Sunday 4 February 2007
Kama ilivyo ada, kumaliza hatua moja ndiyo mwanzo wa kuingia nyingine. Baada ya kumaliza hatua ya Uongozi, juma hili tunaingia kipengele kingine cha UANAJUMUIYA na NEMBO ya Jumuiya. Katika UANAJUMUIYA tutazungumzia suala zima la ushiriki wa mtu katika Jumuiya kwamba:-


1. Je mwanajumuiya ni nani? mtu yeyote mwenye blogu au hata asiyekuwa na blogu?

2. Je tunahitaji taratibu zozote za mtu kujiunga na jumuiya? Je ni zipi hizo?

3. Kuwe na taratibu zozote za mwanajumuiya kutolewa katika Jumuiya? Taratibu gani?

4. Je kuna haja ya kuweka mipaka yoyote ya kinidhamu kwa mwanablogu? ipi?

Pamoja na kujadili suala la uanajumuiya, pia kamati imeona ni vyema kulijadili suala la Nembo ya Jumuiya katika kipindi hiki, sababu ni kwa vile Nembo ni mchoro unaohitaji kubuniwa, hivyo ni bora kazi hii itangazwe mapema ili wenye vipaji vyao waanze kushusha vitu. Mada hii ya Nembo iko huru haifungwi na muda wa juma moja inaweza ikawasilishwa wakati wowote wakati mijadala mingine ikiendelea.

Wachangiaji karibuni tena. Na wachoraji mko huru kuanza kazi ya Nembo.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 2/04/2007 | Maoni: 25

Muundo wa Uongozi uliokubalika.

Haya wanablogu. Ni wakati mwingine tena umewadia wa kutoa jibu lililokubakika katika mada tuliyokuwa tukiijadili. UONGOZI.

Kama wote tunavyojua, tulianza kwa kutafuta jina la Jumuiya, na kufuatia kuchanganua jinsi muundo wa jumuiya utakavyokuwa. Suala la muundo kwa ujumla ni pana na lenye vipengele vingi. Mwanzoni tuliliweka suala hili zima zima, lakini ikaonekana ingekuwa bora kulichanganua kulingana na vipengele vyake na kila kipengele kijadiliwe peke yake.

Mawazo yalikubalika, na kipengele cha UONGOZI kilikuwa cha kwanza kujadiliwa. Kipengele hiki kilipata majuma mawili mazima. Wachangiaji wametoa mawazo yao na hivi ndivyo ilivyokubalika:-

Jumuiya itakuwa na,

1. Mwenyekiti.
2. Katibu.
3. Mweka hazina
4. Kamati mbalimbali.

Katika kipengele cha nne hapo juu cha KAMATI, kutakuwa na kamati zifuatazo:-

1. Kamati ya harakati
2. Kamati ya teknolojia
3. Kamati ya Ufundi
4. Kamati ya picha
5. Kamati ya maadili na sheria
6. Kamati ya uenezi na uhamasishaji

Pamoja na hayo yote, pia kutakuwa na kitengo cha USHAURI na cha KAZI ZA KUJITOLEA.

Vilevile kuna jambo la maana sana lilijitokeza katika juma la majadiliano juu ya uongozi. Jambo hili ambalo Michuzi aliliibua ni juu ya kuwa na NEMBO na BENDERA ya Jumuiya. Jambo hili limekubalika na litatangazwa rasmi ili wajuzi wajitokeze na kuanza kulifanyia kazi. Lakini ikumbukwe ni kazi ya kujitolea bila malipo.

Wanablogu tunashukuru kwa ushirikiano wenu na kaeni chonjo kusikiliza mada itakayofuatia kuanzia juma la kesho.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 2/04/2007 | Maoni: 8

Mjadala juu ya mada ya UONGOZI umeongezeka.

Sunday 28 January 2007
Ndugu wanablogu, kutokana na unyeti wa suala zima la uongozi, kamati ya uongozi wa muda imekubali ushauri uliotolewa mwandani, kwamba muda zaidi uongezwe wa kujadili na kuipanga mada hii ya uongozi. Muda ulioongezwa ni juma moja, hivyo wanablogu tujitahidi kuutumia muda huu vizuri ili itakapofikia mwishoni mwa juma tuwe tumepata jawabu.

Pamoja na hilo, suala la kamati limejitokeza pia katika majadiliano yaliyopita. Suala hili ni muhimu sana ili kuunda uongozi uliokamilika. Hivyo basi katika kipindi hiki kilichoongezwa tutajadili pia kamati zitakazounda jumuiya yetu.

Hadi sasa kamati zilizopendekezwa ni pamoja na :-

1. Kamati ya maadili,
2. kamati ya ufundi na teknolojia
3. Kamati ya uhamasishaji,
4. Kamati ya Jamii (Watoto yatima),
5. Kamati ya sheria.

Bado tunahitaji michango zaidi ili kukamilisha mada hii.

Karibuni uwanjani.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 1/28/2007 | Maoni: 15

Uongozi wa Jumuiya ya wanablogu Tanzania

Tuesday 23 January 2007
Kutokana na ushauri wa mwanaharakati Ndabuli na wengine wote waliounga mkono hoja aliyotoa, (fungua hapa usome alichokisema) kamati ya muda imeona ni kweli kabisa kwamba mada hii ya uongozi ni nzito na yenye vipengele vingi kuweza kujadiliwa yote katika juma moja. Hivyo basi mada hii tunaiweka huru ndani ya majuma manne au zaidi kulingana na vipengele vyake. Hadi sasa hivi tunavipengele vinne vikuu ambavyo ni UONGOZI, UANAJUMUIYA, KATIBA na IDARA kila kipengele kimepewa juma zima kujadiliwa.

Haya, bila kuchelewa tutaanza na kipengele cha UONGOZI.

- je tunataka uongozi wa Jumuiya uweje? kuwe na Mwenyekiti au Rais,
- Kuwe na uongozi wa muda au wa kudumu?
- Viongozi watakuchaguliwa vipi? n.k

Uwanja uko wazi karibuni.

*Shukrani sana Ndabuli. Wanablogu tusihofu kutoa ushauri popote pale tunapodhani panahitaji kuwekwa sawa. Maendeleo hayaji pasipo kubadilishana mawazo.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 1/23/2007 | Maoni: 21

Muundo wa Jumuiya ya Wanablogu Tanzania.

Monday 22 January 2007
Baada ya kupata jina la Jumuiya yetu, sasa tunaingia hatua ya pili. Juma hili tutajadili suala zima la MUUNDO wa Jumuiya yetu. Hapa tutajadili vitu kama:-

1. Uongozi,
- je tunataka uongozi wa Jumuiya uweje? kuwe na Mwenyekiti au Rais,
- Kuwe na idara au wizara zozote?
- Kuwe na uongozi wa muda au wa kudumu?
- Viongozi watakuchaguliwa vipi? n.k

2. Wanajumuiya,
- Je mwanajumuiya ni nani? mtu yeyote mwenye blogu au hadi aombe kuingia katika
Jumuiya?
- Kuwe na taratibu zipi za mtu kujiunga na jumuiya? (sifa)
- Kuwe na taratibu zipi za mwanablogu kutolewa katika Jumuiya?
- Je kuna haja ya kuweka mipaka yoyote ya kinidhamu kwa mwanablogu? ipi?

3. Katiba.
- Je tunahitaji kuwa na katiba?

Hivyo basi wanablogu, juma hili hayo ndiyo tutakayoyajadili, kumbuka hivyo ni vidokezo tu, kama utakuwa na jambo lolote la nyongeza katika hayo basi usisite kuongeza.

Hatua hii ni muhimu sana kwani ndiyo itakayotupelekea kujenga katika yetu kama tuahitaji kuwa na katiba.

Karibuni tena uwanjani.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 1/22/2007 | Maoni: 9

Jina lililokubalika.

Kamati ya muda inachukua nafasi hii kufunga mjadala juu ya JINA la jumuiya tunayotaka kuiunda ya wanablogu wa Tanzania. Mada ilikuwa hewani kwa muda wa juma zima, tunasema asante kwa wote waliochangia kwani wamesaidia kupiga hatua moja mbele. Hadi wakati huu tumekwisha kupata jina la Jumuiya yetu, ambayo kwa mawazo ya wengi wamependekeza iitwe "JUMUIYA YA WANABLOGU TANZANIA. Kamati ya muda haina budi kukubaliana na maoni ya wengi. Hivyo basi Jumuiya yetu itaitwa "JUMUIYA YA WANABLOGU TANZANIA.

Asanteni sana.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 1/22/2007 | Maoni: 5

Utangulizi.

Saturday 13 January 2007
Wasomaji,

Baada ya muda kupita tangu kufanyika kwa mkutano wa blogu Tanzania, kamati ya muda imeamua kufungua blogu hii ili kutoa nafasi kwa kila mtu kuchangia mawazo yake juu ya yale tuliyokubaliana kuyafanyia kazi.

Katika mkutano huo tulikubaliana kuyafanyia kazi masuala makuu yafuatayo:-

1. Uundaji wa jumuiya ya wanablogu Tanzania.

2. Jina la jumuiya na aina ya muundo wake.

3. Kikusanya habari na jina lake.

4. Ujenzi wa tovuti ya jumuiya.

5. Tuzo na mfumo wa utolewaji wake.

6. Siku ya blogu Tanzania.

Ili kuweza kupata mawazo ya kina, kamati ya muda imepanga kwamba iwe ikijadiliwa mada mojamoja katika kipindi cha juma zima, na baada ya hapo tunahitimisha mada kwa kuchagua mapendekezo ya wengi kuwa jibu la mada.

Kwa kuanza, tunaanza kwa kupendekeza JINA la Jumuiya ya blogu Tanzania.
Wewe mwanablogu ungependa Jumuiya iitweje? Kumbuka mada hii itakuwa hewani hadi Ijumaa, Jumapili litapatikana jibu na jumatatu itatangazwa mada inayofuatia.
 
© Blogu Tanzania | Tarehe: 1/13/2007 | Maoni: 15